Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Michezo ni Uchumi: RC Mgumba
Oct 04, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Omary Mgumba amesema michezo hukuza uchumi wa nchi ambapo kwa sasa wanamichezo zaidi ya timu 50 kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara wapo mkoani hapo wakishiriki kwenye michezo ya Shirikisho la michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI).

Mhe. Mgumba akiwa miongoni mwa wachezaji wa Timu ya RAS Tanga kwenye mchezo wa soka uliochezwa kwenye uwanja wa Mkwakwani Oktoba 04, 2022 jijini Tanga ambapo timu yake imefungwa na Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara kwa magoli 2-1, ambapo amesema ulikuwa mzuri kwa kuwa wachezaji wameonesha juhudi na uungwana.

“Michezo hii ni kwa ajili ya watumishi wa umma kama mlivyoona watumishi wanatoka nchi nzima tumekutana hapa kwa ajili ya michezo hii, imeleta faida kubwa kwa watumishi wenyewe kwa sababu inaleta umoja mshikamano na inaleta afya ya akili, michezo inalisha akili na miili yetu” amesema Mkuu huyo wa Mkoa wa Tanga.

Mhe. Mgumba amesisitiza kuwa michezo ina faida kwa kuwa michezo inaondoa stress na watumishi wamepata mtoko kwa kusafiri kutoka sehemu moja kwenda Tanga kujifunza mambo mbalimbali ambayo Mkoa wa Tanga umejaliwa.

“Wachezaji hawa wanakaa zaidi ya siku 15, wanakula wanalala, hivyo wenye nyumba za kulala wageni, wanatumia usafiri wa vyombo mbalimbali vya usafiri, hoteli, migahawa wote wanafanya biashara na wanatengeneza uchumi wa Tanga na Taifa”, amesema Mhe. Mgumba.

Aidha, amewashukuru Viongozi wa Serikali wakiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia na kuwapa vibali watumishi kushiriki mashindano ya SHIMIWI 2022 jijini Tanga kwa kuwa michezo ni watu na watu ndiyo watumishi hao na wananchi wa Jiji la Tanga na viunga vyake ambao mara zote wamejitokeza kushuhudia mashindano hayo katika viwanja mbalimbali inapochezwa michezo hiyo. 

Akizungumzia ushindi wa mabao 2-1 waliopata, Kaimu Mkurugenzi Idara ya Utawala na Rasilimali Watu, Bi. Veronica Nchango kutoka Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara amesema wizara hiyo imejipanga vizuri kwenye mashindano hayo kwa kuwa tayari wameshinda mechi mbili na wametoa suluhu mchezo mmoja na wanatarajia kuibuka na ushindi kwenye mchezo uliobaki dhidi ya timu ya RAS Mara.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi