Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Mavunde Abainisha Vipaumbele Sekta ya Madini 2030
Sep 11, 2023
Mavunde Abainisha Vipaumbele Sekta ya Madini 2030
Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde akizungumza katika Mkutano na Wachimbaji Wadogo wa madini kutoka Shirikisho la Wachimbaji wadogo wa Madini Tanzania (FEMATA) uliofanyika jijini Dodoma
Na Mwandishi Wetu

Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde amebainisha vipaumbele vyake katika Sekta ya Madini ili kuhakikisha taifa linanufaika na uwepo wa Madini yanayopatikana hapa nchini huku akitaja  Maono ifikapo mwaka 2030  kuwa madini ni Maisha na Utajiri.

Amebainisha hayo leo septemba 11 , 2023 wakati akizungumza katika Mkutano  na  Wachimbaji Wadogo wa madini kutoka   Shirikisho la  Wachimbaji wadogo wa  Madini Tanzania (FEMATA) uliofanyika jijini Dodoma.

Akizungumzia juu ya kuongeza taarifa za utafiti wa  jiolojia Mhe. Mavunde amesema moja ya vipaumbele vyake katika sekta ya madini ni kuijengea uwezo Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) ili iweze kufanya utafiti wa kina kwa ndege yaani (Air Born Geophysical Survey) utakaotoa taarifa zitaonesha utajiri wa madini yaliyopo nchini kwa kiwango kikubwa tofauti na sasa ambapo ni  asilimia 16 tu ya eneo lote nchi nzima limefanyiwa utafiti wa kina.

Waziri Mavunde amesema  GST inapaswa kufanana na taasisi zote za Utafiti wa Madini duniani ikiwa na  maabara ya kisasa itakayotumiwa na wachimbaji wote nchini.

“Ndugu zangu tukipiga picha ya miamba yote nchi nzima, tutapata taarifa sahihi ya kijiolojia ili wachimbaji wasifanye kazi zao kwa kubahatisha , uchimbaji ni Sayansi sio bahati wala uchawi, mchimbaji mwenye taarifa  ya utafiiti wa kijiolojia atafanikiwa zaidi kupitia Sekta hii ya Madini,”amesema Mhe. Mavunde.

Aidha, ametaja mpango mwingine kuwa Wizara itaenda kuwa na makumbusho ya madini  ili wananchi wapate kuona na kufahamu madini yanayopatikana  nchini kuliko kuyasikia tu.

Akizungumzia kuhusu utoroshaji wa madini Mhe. Mavunde ametaja  mkakati wa kutokomeza utoroshaji wa madini nchini ili madini yote yaliyopo kwenye mnyororo wa biashara ya madini yaonekane na yalete faida kwa taifa.

Amesema kuwa mtihani wake wa kwanza kama Waziri wa Madini ni kuhakikisha Wizara inakusanya shilingi trilioni 1 kwa Mwaka wa Fedha 2023/24 hivyo suala la utoroshaji madini halina nafasi.

“Kuhusu utoroshaji naomba tushirikiane ntasimamia sheria,  sitasita kuwachukulia hatua wale wote wanatorosha madini, sitaangalia sura ya mtu, mtahakikisha nasimamia kwa dhati na naamini kwa kushirikiana tutafanikisha kumaliza kabisa hilo tatizo, mimi na wenzangu tutakuwa wakali sana katika hili, milango yangu itakuwa wazi tushirikiane,” amesema Mavunde.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi