[caption id="attachment_27162" align="aligncenter" width="750"]
Na: Fatma Salum
Chama cha Maafisa Habari na Mawasiliano Serikalini (TAGCO) kwa kushirikiana na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo wameandaa kikao kazi cha Maafisa Habari na Mawasiliano wa Taasisi zote za Serikali kwa lengo la kuwajengea uwezo ili waweze kutangaza kwa weledi shughuli za Serikali.
Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa Chama hicho Bw. Paschal Shelutete wakati akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam kuhusu kikao kazi hicho kinachotarajiwa kufanyika Mkoani Arusha kuanzia Machi 12 hadi 16 mwaka huu.
[caption id="attachment_27163" align="aligncenter" width="750"]“Kikao kazi hiki ni cha 13 katika mfululizo wa vikao vinavyofanyika kila mwaka kwa lengo la kuwajengea washiriki uwezo wa namna ya kutangaza shughuli za Serikali na kuhakikisha Idara na Vitengo vya Mawasiliano na Uhusiano Serikalini vinaimarishwa ili kuendana na kasi ya utendaji wa Serikali ya Awamu ya Tano,” alisisitiza Shelutete.
Alifafanua kuwa washiriki wa kikao kazi hicho ni Maafisa Habari, Mawasiliano, Uhusiano na Itifaki kutoka kwenye Wizara, Idara zinazojitegemea, Taasisi, Wakala wa Serikali, Mamlaka, Halmashauri za Miji, Manispaa, Majiji na Mikoa.
[caption id="attachment_27165" align="aligncenter" width="750"]Pia Shelutete alieleza kuwa katika kikao kazi hicho, jumla ya mada 14 zitawasilishwa ambazo zitajikita zaidi kwenye masuala mbalimbali yahusuyo habari, mawasiliano, uhusiano na itifaki.
“Maafisa Habari, Mawasiliano, Uhusiano na Itifaki wanahimizwa kuthibitisha ushiriki wao kabla ya tarehe 7 Machi, 2018,” alisisitiza.
TAGCO ni chama kilichoanzishwa rasmi mwaka 2012 na kusajiliwa kwa mujibu wa sheria za nchi. Kila mtumishi wa umma anayeshughulika na masuala ya habari na mawasiliano anapaswa kuwa mwanachama wa TAGCO.