Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Falsafa ya Dkt. Ndumbaro ni Bidii ya Kazi, Umoja na Ustawi wa Watumishi
Sep 04, 2023
Falsafa ya Dkt. Ndumbaro ni Bidii ya Kazi, Umoja na Ustawi wa Watumishi
Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro akikabidhiwa ofisi na Ilani ya Uchaguzi ya 2020-2025 ikiwa ni ishara ya kupokea Ofisi kutoka kwa aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo Balozi, Dkt. Pindi Chana ambaye sasa ni Waziri wa Katiba na Sheria Septemba 4, 2023 Jijini Dodoma.
Na Eleuteri Mangi, WUSM, Dodoma

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro amesema falsafa yake katika kutekeleza majukumu yake ni bidii katika kazi, kufanya kazi kwa umoja pamoja na ustawi wa watumishi.

 

Waziri Dkt. Ndumbaro amesema hayo Septemba 04, 2023 wakati wa makabidhiano ya ofisi ya Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo na aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo, Balozi Dkt. Pindi Chana ambaye amehamishiwa Wizara ya Katiba na Sheria.

 

“Falsafa yangu katika kazi ina mambo matatu, ‘hard work’, kwenye kazi mimi ni mtu wa kazi kazi, ‘team work’, kufanya peke yako haina maana, kufanya kazi kwa pamoja tutafika mbali na kwa ufanisi, na ‘welfare’, sote tuna kila sababu ya kufurahia matunda ya kazi yetu”, amesema Dkt. Ndumbaro.

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Katiba na Sheria, Balozi Dkt. Pindi Chana (wa tatu kutoka kulia), Naibu Waziri wa wizara hiyo, Mhe. Hamis Mwinjuma (wa pili kushoto), Katibu Mkuu Bw. Saidi Yakubu (kushoto) na Naibu Katibu Mkuu, Bw. Nicholaus Mkapa (kulia) mara baada ya kuwasili ofisini Mtumba jijini Dodoma Septemba 4, 2023.

 

Aidha, Dkt. Ndumbaro amesema kuwa hajawahi kupokelewa kwa bashasha tangu ameanza kufanyakazi baada ya kuteuliwa kutumikia wizara mbalimbali na kuongeza kuwa amepata pongezi kutoka taasisi mbalimbali na wadau hatua inayoonesha watu wana matumaini kwa kuteuliwa kwake kuiongoza wizara ambapo amewasihi menejimenti na watumishi wa wizara hiyo kutekeleza majukumu yao ili kuwahudumia watanzania.

 

Akikabidhi ofisi, Waziri Balozi Dkt. Pindi Chana ambaye amehamishiwa Wizara ya Katiba na Sheria amesema kuwa Wizara hiyo inawawakilishi kila wilaya na mikoa yote nchi nzima maafisa Utamaduni na Michezo ambao wanawahudumia watanzania katika sekta za Utamaduni, Sanaa na Michezo.  

 

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma amesema kuwa hiyo ni Wizara ya furaha ambapo amesisitiza kuwa wakati watu wanaburudika, viongozi na watumishi wa wizara hiyo wanakuwa kazini kutekeleza majukumu yao pamoja wadau.

 

Awali akimkaribisha Mhe. Waziri, Dkt. Ndumbaro, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Bw. Saidi Yakubu ametoa kwa ufupi wasifu wa Dkt. Ndumbaro na kusisitiza kuwa Waziri huyo ni mtendaji mzuri na mdau mkubwa wa michezo wa miaka mingi na ni mwanamichezo mzuri wa mchezo wa gofu ambapo amemuahidi kuwa atapata ushirikiano kwani menejimenti na watumishi wa wizara hiyo wapo tayari kupokea maelekezo atakayotoa na kuyatekeleza.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi