Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Dkt. Ndumbaro: Haikuwa Kazi Rahisi Kushinda Kuandaa AFCON 2027
Sep 29, 2023
Dkt. Ndumbaro: Haikuwa Kazi Rahisi Kushinda Kuandaa AFCON 2027
Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro akizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo pichani) leo jijini Dar es Salaam kuhusu nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki kuandaa Fainali za Mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027).
Na Eleuteri Mangi, WUSM, Dar es Salaam

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro amesema haikuwa kazi rahisi kwa nchi za Tanzania, Kenya na Uganda kushinda zabuni ya kuandaa Fainali za Mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027). 

Dkt. Ndumbaro amesema hayo Septemba 29, 2023 jijini Dar es Salaam alipokuwa kwenye mkutano na Waandishi wa Habari kuhusu nchi hizo za Jumuiya ya Afrika Mashariki kuandaa mashindano hayo makubwa barani Afrika.

“Haikuwa kazi ndogo, ilikuwa kazi ngumu sana, tuliweka mikakati ya pamoja ya kutosha kuhakikisha zabuni yetu ambayo sasa ni EA Pamoja AFCON 2027 inashinda. Mipango yetu ilikuwa na nguvu na msukumo wa Marais wetu watatu; Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mhe. Dkt. William Samoye Ruto na Mhe. Jenerali Yoweri Kaguta Museveni utayari na mchango wao kwenye mashindano haya kwetu ulikuwa mtaji wa kwanza”, amesema Dkt. Ndumbaro.

Dkt. Ndumbaro amesema Wizara itatekeleza maelekezo yote yaliyotolewa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kujenga viwanja vipya viwili na kusisitiza maandalizi mengine yafanyike haraka na kwa wakati ili Watanzania wanufaike.

Vigezo ambavyo vimetumika kushinda zabuni hiyo ni pamoja na Serikali zote tatu ziwe na dhamana ya Dola za Marekani milioni 30 kwa kila nchi ambapo jumla yake ni Dola za Marekani milioni 90, viwanja sita vya mashindano na kila nchi inapaswa kuwa na angalau viwanja viwili ambapo kwa Tanzania upo Uwanja wa Benjamin Mkapa umekidhi sifa na unaendelea kufanyiwa ukarabati wa awamu ya kwanza, Uwanja wa Aman Zanzibar, huu unaendelea na maboresho huku Uwanja mpya wa Arusha unatarajiwa kujengwa na kukamilika kabla ya mashindano ya AFCON 2027.

Kwa upande wake Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini, Bw. Wallace Karia amesema anawashukuru mawaziri wote wa michezo, Mhe. Dkt. Damasi Ndumbaro, Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Tanzania, Mhe. Ababu Namwamba, Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Kenya na Mhe. Peter Ogwang, Waziri wa Nchi, Elimu na Michezo, Uganda kwa kazi kubwa waliyoifanya kufanikisha ushindi huo na nchi hizo kupewa dhamana ya kuwa mwenyeji wa AFCON 2027.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi