Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Dkt. Nchemba Akutana na Shirika la EKN Lililotoa Fedha Ujenzi wa SGR
Sep 26, 2023
Dkt. Nchemba Akutana na Shirika la EKN Lililotoa Fedha Ujenzi wa SGR
Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba akiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Bima la Dhamana la nchi ya Sweden, (EKN), Bi. Anna-Karin Jatko, mjini Stockholm, Sweden, ambalo limetoa usaidizi katika ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) upande wa malighafi ya ujenzi, vitendea kazi, mifumo ya umeme, mitambo na teknolojia ambapo ameishukuru Sweden kupitia Taasisi zake likiwemo Shirika hilo la Bima la Dhamana (EKN), kwa ushirikiano wake madhubuti na kuchangia maendeleo ya Tanzania, ikiwemo ujenzi wa mradi wa Reli ya Kisasa SGR kutoka Dar es Salaam hadi makutupora mkoani Singida.
Na Benny Mwaipaja, Stockholm, Sweden

Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, ameishukuru Sweden kupitia Taasisi zake likiwemo Shirika la Bima la Dhamana la nchi hiyo (EKN), kwa ushirikiano wake madhubuti na kuchangia maendeleo ya Tanzania, ikiwemo ujenzi wa mradi wa Reli ya Kisasa SGR kutoka Dar es Salaam hadi makutupora mkoani Singida.

Dkt. Nchemba, amesema hayo Mjini Stockholm nchini Sweden alipokutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo,  Bi. Anna-Karin Jatko,  ambalo limetoa Dhamana kwa mabenki mbalimbali yanayotoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR).

Aidha katika mradi huo, nchi ya Sweden kupitia kampuni zake imeshiriki katika kuleta malighafi za ujenzi, vitendea kazi, mifumo ya umeme na mawasiliano, mitambo na teknolojia, na katika masuala ya  mazingira na jamii kwa mujibu wa viwango vya kimataifa 

Alisema kuwa miradi ambayo Sweden imeisaidia Tanzania tangu kuanza kwa ushirikiano kati ya nchi hizo mbili katika nyanja za kiuchumi na kijamii, ikiwemo, afya, maji, nishati, uchumi jumuishi wa kifedha, pamoja eneo la usafirishaji,  imekuwa na manufaa makubwa kwa watanzania.

Alisema kuwa ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) unaendelea vizuri na kwamba Serikali inakamilisha baadhi ya taratibu za mazingira na jamii kwa mujibu wa viwango vya kimataifa  ili kukamilisha taratibu za upatikanaji wa rasilimali  fedha kwa kipande cha tatu na ya nne. 

Nchi hiyo pia ilitoa Dhamana kwa ajili ya upatikanaji fedha kwa kipande cha kwanza na pili ya SGR kutoka Dar es Salaam-Morogoro hadi Makutupora-Mkoani Singida, ambao ujenzi wake umefikia asilimia 98 kwa lot ya kwanza na asilimia 95 kwa lot 2 na inatarajiwa majaribio ya uendeshaji kuanza mapema mwezi Disemba, 2023.

“Reli hii yenye urefu wa kilometa 2,102 ni muhimu kwa maendeleo na uchumi wa nchi na ni mradi wa kimkakati wa kikanda na ni kipaumbele cha nchi kwa hivi sasa kwa sababu utakuwa na matokeo makubwa kijamii na kiuchumi utakapo kamilika.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Bima la Dhamana la Sweden (EKN), Bi. Anna-Karin Jatko, alisifu maendeleo makubwa ambayo Tanzania imepiga kiuchumi na kijamii ambapo usimamizi mzuri wa uchumi, maboresho yaliyofanyika katika mazingira ya uwekezaji na ufanyaji biashara yanaleta mwanga mkubwa wa maendeleo na kwamba Sweden inaunga mkono na iko tayari kuendelea kuisaidia Tanzania ili itimize malengo yake ya kuwaletea maendeleo wananchi wake.

Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba na ujumbe wake wako katika ziara ya kikazi katika baadhi ya nchi za Scandinavia ambapo lengo la ziara hiyo ni kuimarisha ushirikiano wa kimkakati wa kiuchumi kati ya Tanzania na nchi hizo.


 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi