Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Dkt. Biteko Aagiza Matumizi Sahihi ya Fedha za Serikali
Sep 24, 2023
Dkt. Biteko Aagiza Matumizi Sahihi ya Fedha za Serikali
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt.Doto Biteko akizungumza na wananchi mara baada ya kuwasili katika Jimbo la Bukombe mkoani Geita tarehe 24 Septemba, 2023 kwa ajili ya ziara ya kikazi.
Na Teresia Mhagama

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko ameanza ziara ya kikazi katika jimbo hilo lililoko mkoani Geita ikiwa ni ziara ya kwanza kufanyika  tangu ateuliwe na kuapishwa na Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati.
 

Mara baada ya kuwasili katika Jimbo hilo tarehe 24 Septemba, 2023, Dkt. Biteko alipokelewa na wananchi wa Jimbo hilo pamoja na viongozi mbalimbali katika Wilaya ya Bukombe na Mkoa wa Geita.
 

Akizugumza katika Mkutano wa hadhara, Dkt. Biteko amemshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kumuamini na kuona kuwa anaweza kumsaidia katika majukumu aliyokabidhiwa na kuahidi kuwa, atatekeleza majukumu yake kwa ufanisi katika kuwatumikia wananchi ili kuitendea haki imani iliyooneshwa kwake.

Amesema kuwa, chini ya uongozi wa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kila kitu kilichopangwa kufanyika  kinaendelea kufanyika kutokana fedha anazotoa katika  miradi ya sekta mbalimbali ikiwemo mradi wa umeme wa Julius Nyerere (MW 2115), ujenzi wa Daraja wa Busisi, ununuzi wa ndege, madarasa, vituo vya afya, utalii n.k.
 

Kutokana na hilo, Dkt. Biteko amewataka watendaji na watumishi nchini kusimamia matumizi sahihi ya fedha za Serikali kwani fedha hizo ndizo zinategemewa na watanzania katika kuwaletea maendeleo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, viongozi wa Mkoa wa Geita wamemshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kumuamini Dkt. Doto Biteko katika nafasi hiyo kubwa na adhimu na kwamba wana imani kuwa ataitendea haki nafasi hiyo kutokana na historia yake ya uchapakazi na uadilifu.

Viongozi hao wakiwemo Wabunge na Wakuu wa Wilaya katika Mkoa wa Geita wamemshukuru Rais. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa barabara wilayani Chato, ujenzi wa Chuo cha VETA wilayani Nyang'hwale na upelekaji umeme vijijini katika  vijiji vya mkoa huo.
 

Kwa upande wake, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde amesifu juhudi zilizofanywa na Dkt. Biteko wakati akihudumu kama Waziri wa Madini  na kueleleza kuwa amesaidia kuinua mchango sekta ya madini katika uchumi wa nchi na ameahidi kuwa ataendeleza misingi hiyo mizuri ikiwemo ya kufanya utafiti wa madini katika eneo lote la nchi ili wachimbaji wachimbe madini kwa uhakika na hivyo kuongeza mapato ya nchi.
 

Aidha, ameendelea kusisitiza kuwa, hatalifanyia mzaha suala la utoroshaji wa madini nchini na kwamba wote watakaotorosha madini watachukuliwa hatua za kisheria kwani wanakosesha nchi mapato.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martine Shigela amemshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha za kugharamia miradi mbalimbali ya maendeleo na huduma za kijamii ikiwemo shule, hospitali  na umeme katika Mkoa wa Geita.
 


 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi