Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Waziri Mkuu Majaliwa Awakaribisha Warusi Kuwekeza Kwenye Sekta ya Reli
Oct 23, 2019
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_48270" align="aligncenter" width="750"] Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Russian Railways, Alexander Misharin kabla ya mazungumzo yao kwenye hoteli ya Marriot ya Sochi nchini Urusi.[/caption]

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Russian Railways, Bw. Alexander Misharin na kumweleza kuwa Tanzania inahitaji sana kuimarisha usafiri wa ndani wa reli hasa katika majiji ya Dar es salaam, Mwanza, Dodoma, Arusha, Mbeya na Tanga.

Amesema kampuni hiyo yenye uwezo mkubwa wa kujenga reli mpya, kukarabati reli, kutengeneza injini za treni na mabehewa pamoja na ukarabati wake inahitajika sana nchini ili kufanikisha mpango wa Serikali wa kuimarisha reli za zamani za TAZARA, Reli ya Kati na kufugua reli ya Kaskazini inayounganisha mikoa ya Dar es salaam, Tanga, Kilimanjaro na Arusha.

Waziri Mkuu alizungumza na Mkurugenzi huo jana (Oktoba 22, 2019) kwenye hoteli ya Marriot iliyopo Sochi nchini Urusi, ambapo alitumia fursa hiyo kuikaribisha kampuni ya Russian Railways kuwekeza nchini hususani katika sekta ya ujenzi, ufundi na mafunzo ikishirikiana na makampuni ya Watanzania.

Waziri Mkuu yuko nchini Urusi kuhudhuria mkutano baina ya Wakuu wa Nchi na Serikali kutoka Mataifa ya Afrika na Urusi (Russia-Africa Summit), unaotarajiwa kuanza leo Oktoba 23 hadi 24, 2019 katika jiji la Sochi. Waziri Mkuu anahudhuria mkutano huo kwa niaba ya Rais, Dk. John Pombe Magufuli.

“Katika kipindi hiki ambacho Tanzania inajenga reli ya kiwango cha kimataifa ya SGR pamoja na kufufua reli ya Kaskazini, inaikaribisha Kampuni ya Russian Railways kwa mikono miwili ije ifanye mazungumzo rasmi na Wizara husika. Pia Serikali inao mkakati wa kujenga reli mpya katika ukanda wa Kusini kutoka Mtwara hadi Ruvuma ili kuiunganisha bandari ya Mtwara na mikoa ya Kusini pamoja na nchi jirani za Malawi na Zambia.”

Alisema Tanzania kwa sasa inahitaji sana kuimarisha usafiri wa ndani wa reli hasa katika majiji ya Dar es salaam, Mwanza, Dodoma, Arusha, Mbeya na Tanga hivyo endapo mazungumzo kati ya Wizara husika na kampuni hiyo yataonekana kuwa na tija na yana maslahi kwa Watanzania, kampuniyo itapewa fursa ya kuwekeza nchini.

Kadhalika, Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo kuwakumbusha wafanyabiashara wa Tanzania, wito wa Rais Dkt. John Pombe Magufuli wa kuwataka watumie fursa lukuki zilizopo nchini kuanzisha makapuni ya pamoja na makampuni ya nje ili kuunganisha nguvu kwa kuendesha kwa pamoja makampuni yatakayoanzishwa.

Alisema utaratibu wa makampuni ya Tanzania kuanzisha makampuni ya pamoja na makampuni ya nje utawapa Watanzania fursa ya kujipatia kipato pia wataweza kulinda maslahi ya Taifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Kapuni ya Russia Railways, Bw. Misharin alimuhakikishia Waziri Mkuu kuwa kampuni yake iko tayari kushirikiana na wafanyabiashara wa Kitanzania katika kuanzisha makapuni ya pamoja ili kuipatia Tanzania tekinolojia ya masuala ya reli na kubadilisha ujuzi.

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi