Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Waziri Mkuu Aungana na Wanasongea Kuomboleza Kifo cha Gama
Nov 26, 2017
Na Msemaji Mkuu

Taarifa Kwa Vyombo Vya Habari

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameungana na wanafamilia, wananchi wa Songea katika kuomboleza kifo cha aliyekuwa mbunge wa jimbo la Songea, Bw. Leonidas Gama, nyumbani kwa marehemu Likuyu wilayani Songea.

Bw. Gama   amefariki dunia jana (Ijumaa, Novemba 24, 2017) katika Hospitali ya Peramiho mkoani Ruvuma alikokuwa akipatiwa matibabu. Marehemu anatarajiwa kuzikwa Jumatatu, Novemba 27, 2017 katika kijiji cha Likuyu wilayani Songea.

Akizungumza kwa niaba ya Serikali, Waziri Mkuu amesema kifo hicho ni pigo kwa Serikali kwa sababu marehemu alishirikiana nayo vizuri tangu akiwa mtumishi wa umma na hata baada ya kuchaguliwa kuwa mbunge wa Jimbo la Songea.

Waziri Mkuu amesema msiba huo umeleta mtikisiko mkubwa kwa sababu baada ya kurudi nchini kutoka India alikokuwa akipatiwa matibabu aliwaeleza kuwa hali yake kwa sasa ni nzuri. ”Ametuachia pengo kubwa ambalo hatuna namna ya kuliziba.”

Ameongeza kuwa alipokea taarifa za msiba huo kwa huzuni na mshtuko mkubwa kwa sababu siku mbili kabla ya Waziri Mkuu kuanza ziara yake mkoani Ruvuma, Bw. Gama alimpigia simu na kumjulisha kwamba yeye anatangulia Songea kumpokea.

“Kifo ni mipango ya Mwenyezi Mungu na kwamba Bw. Gama ametangulia nasi tutafuata, hivyo wajibu wetu sote ni kumuombea kwa Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema. Gama alikuwa kiongozi na mwanga wa maendeleo.”

Pia Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo kuwaomba wanafamilia, mke wa marehemu na watoto na wananchi wa jimbo la Songea waendelee kuwa watulivu na wavumilivu katika kipindi hiki kigumu cha kuondokewa na mpendwa wetu.”

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Bibi Christine Mndeme alimshukuru Waziri Mkuu kwa kutenga muda wake na kwenda kuwafariji wafiwa licha ya majukumu mengi na makubwa aliyonayo.

Awali msemaji wa familia Bw. Issa Fusi alimshukuru Waziri Mkuu pamoja na viomgozi mbalimbali waliojitokeza na kuwafariji baada ya kutokea kwa msiba huo.”Kaka yetu tulimpenda sana kazi ya Mungu haina makosa.”

IMETOLEWA NA:

OFISI YA WAZIRI MKUU, 

JUMAMOSI, NOVEMBA 25, 2017.

     

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi