Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Waziri Mchengerwa Awakabidhi Kombe la UEFA Mashabiki wa Real Madrid
May 29, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Na John Mapepele


Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe, Mohamed Mchengerwa amewakabidhi kombe la UEFA mashabiki wa timu ya Real Madrid baada ya timu hiyo kutwaa ubingwa usiku wa kuamkia leo huku akisisitiza kuwa Wizara yake itaendelea kuwa bunifu kwenye sekta za Utamaduni, Sanaa na Michezo ili kuwapa furaha watanzania.


Mhe. Mchengerwa amesema hayo kwa wapenzi soka katikati ya Daraja  la Tanzanite jijini Dar es Salaam kwenye tukio maalum la kuangalia mubashara fainali za UEFA lililoratibiwa na kampuni ya kinywaji cha Heineken kwa  kushirikiana na Wizara  ya Utamaduni, Sanaa na Michezo usiku wa kuamkia leo.


Katika fainali hii timu ya Real Madrid imeibuka bingwa wa  kombe la UEFA wa mwaka huu baada ya kuibamiza Liverpool bao moja katika kipindi cha pili cha mchezo.


Ameongeza kuwa  sekta za Utamaduni, Sanaa na Michezo ndiyo nguvu shawishi za taifa lolote duniani.


Amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mhe, Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya ya kuitangaza na kuifungua Tanzania duniani kupitia Filamu ya Royal Tour.


Kabla ya mechi hiyo mamia ya watu waliohudhuria waliopata fursa ya kuangalia Filamu hiyo ya Royal Tour.


Ameongeza kuwa Wizara kwa kushirikiana na wadau wataratibu tukio maalum la kuionesha  Filamu ya Royal Tour kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja jijijini ili wananchi wengi waweze kupata fursa ya kuiangalia.


Aidha, amewataka wadau mbalimbali wa sekta za Utamaduni, Sanaa na Michezo kuendelea  kushirikiana na Wizara katika kuleta mapinduzi makubwa kwenye sekta hizo.


Kwa upande wake, Mwakilishi wa Kampuni ya kinywaji cha Heineken nchini ambayo ndiyo aliyedhamini kuonyesha mubashara fainali hizo hapa nchini kupitia DSTv amesema wataendelea kushirikiana na Serikali katika kuendeleza Sekta za Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa faida wananchi wa Tanzania.


Katika tukio hilo Mhe. Waziri aliambatana na Katibu Mkuu, Dkt. Hassan Abbasi, Naibu Katibu Mkuu, Saidi Yakubu na Watendaji wengine wa Wizara hiyo.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi