Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Waziri Hasunga Aitaka TARI Kufanya Tafiti Zinazolenga Kuongeza Tija
Jun 18, 2020
Na Msemaji Mkuu

Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga akikagua mashamba ya maonesho wakati wa hafla ya ufunguzi wa maonesho ya Kilimo Bishara mwaka 2020 yaliyoandaliwa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI-Ilonga) kwa kushirikiana na makampuni ya mbegu tarehe 17 Juni 2020. 

Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Morogoro

Katika Kipindi cha Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt. John Pombe Magufuli uzalishaji wa chakula umeendelea kuimarika na hivyo kuiwezesha nchi yetu kujitosheleza kwa chakula kwa asilimia 100 na kuwa na ziada ya takribani tani milioni 2.8 ambayo huuzwa nje ya nchi.

Pamoja na mafanikio hayo, bado kilimo kina changamoto mbalimbali zikiwemo matumizi hafifu ya pembejeo (mbegu bora, mbolea, viuatilifu), mabadiliko ya tabia nchi (ukame na mafuriko) ambayo husababisha kuibuka kwa aina mpya ya visumbufu vya mazao na upungufu wa rutuba ya udongo (magadi∕chumvi katika udongo, tindikali), na upotevu wa mazao baada ya mavuno, masoko na ukosefu wa mitaji kwa wakulima walio wengi.

Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga ameyasema hayo tarehe 18 Juni 2020 wakati akizungumza kwenye ufunguzi wa maonesho ya Kilimo Bishara mwaka 2020 yaliyoandaliwa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI-Ilonga) kwa kushirikiana na makampuni ya mbegu tarehe 17 Juni 2020 huku akiitaka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) Kufanya tafiti zinazolenga kuongeza tija ya uzalishaji pamoja na Uhamasishaji  wa matumizi ya pembejeo za kilimo: kwa kutoa elimu kupitia mashamba darasa, maonesho ya kilimo, vyombo vya habari mbalimbali  juu ya kanuni za kilimo bora  ili kuongeza tija.

Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga akikagua mashamba ya maonesho wakati wa hafla ya ufunguzi wa maonesho ya Kilimo Bishara mwaka 2020 yaliyoandaliwa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI-Ilonga) kwa kushirikiana na makampuni ya mbegu tarehe 17 Juni 2020. 

Waziri Hasunga ameitaka TARI Kuhaulisha teknolojia rafiki kwa kuzingatia jinsia katika uzalishaji na usindikaji mazao kwenye mnyororo wa thamani pamoja na Kushirikisha wadau mbalimbali kutoka sekta za umma na binafsi kufikisha kwa kasi matokeo ya tafiti kwa walengwa.

Katika maonesho hayo yenye kauli mbiu isemayo “Mapinduzi yenye tija kwa kilimo endelevu kupitia ubunifu, uwekezaji na biashara” Waziri Hasunga ameeleza kuwa kilimo ni sekta muhimu katika maendeleo ya uchumi wa Wananchi na Taifa, hususani katika kuufikia uchumi wa kati ambao msingi wake mkubwa ni viwanda.

Amezitaja Takwimu za mwaka 2018 zinaonesha kwamba kilimo kinaajiri takribani asilimia 58 ya watanzania na kinachangia asilimia 28.2 kwenye pato la taifa. Kati ya asilimia hizo sekta ndogo ya mazao inachangia asilimia 16.2 ya uchumi wa Taifa.

Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga akikagua mashamba ya maonesho wakati wa hafla ya ufunguzi wa maonesho ya Kilimo Bishara mwaka 2020 yaliyoandaliwa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI-Ilonga) kwa kushirikiana na makampuni ya mbegu tarehe 17 Juni 2020. 

Aidha, Waziri Hasunga amesema kuwa kati ya mwaka 2015 na 2019 sekta ya kilimo imeendelea kukua kwa wastani wa asilimia 5.2, ambapo sekta ndogo ya mazao imeendelea kukua kwa wastani wa asilimia 5.8. Kilimo pia kinachangia maendeleo ya viwanda kwa kuwezesha upatikanaji wa malighafi kwa zaidi ya asilimia 65.

Kadhalika, Hasunga ameitaka Taasisi hiyo ya utafiti wa Kilimo Tanzania kujitangaza kwani imegundua mbegu bora nyingi sana, lakini wakulima hawazijui na hazijawafikia. “Rai yangu kwenu TARI na Wadau wa utafiti wa kilimo ni kwamba, mjaribu kuhakikisha teknolojia mnazozigundua zinawafikia walengwa ambao ni wakulima” Amesisitiza Waziri Hasunga

WAziri Hasunga ameeleza kuwa Wizara ya Kilimo kupitia TARI na washiriki wote wa maonesho hayo wamejizatiti vilivyo kuchangia katika juhudi za Serikali kufikia uchumi wa kati na kuendana na Sera na Mipango ya Serikali hii ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ya kufikia uchumi wa kati kupitia viwanda ifikapo 2025.

Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga akikagua mbegu zinazozalishwa na Wakala wa Mbegu Tanzania (ASA) wakati wa hafla ya ufunguzi wa maonesho ya Kilimo Bishara mwaka 2020 yaliyoandaliwa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI-Ilonga) kwa kushirikiana na makampuni ya mbegu tarehe 17 Juni 2020. 
Sehemu ya wakulima wakazi wa Kilosa mkoani Morogoro wakifatilia hotuba ya Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga wakati wa ufunguzi wa maonesho ya Kilimo Bishara mwaka 2020 yaliyoandaliwa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI-Ilonga) kwa kushirikiana na makampuni ya mbegu tarehe 17 Juni 2020. 
 (Picha Zote Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo)

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi