Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Watanzania Wapya Kutoka Burundi Watakiwa Kuishi kwa Kuzingatia Katiba na Sheria za Tanzania
Oct 18, 2018
Na Msemaji Mkuu

Na Tiganya Vincent - RS Tabora

Waliokuwa wakimbizi ambao wamepata uraia wa Tanzania wametakiwa kujifunza Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuzingatia sheria za nchi ili kuepuka kujiingiza katika vitendo vya kihalifu ambavyo vitawaondolea sifa ya kuendelea kuwa Watanzania.

Kauli hiyo imetolewa jana mjini hapa na Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri wakati akifunga mkutano wa siku mbili wa mrejesho wa tathmini ya juu ya mambo makuu yanayowakabili Watanzania wapya wanaoishi Ulyankulu, Mishamo na Katumba.

Alisema Serikali haitamvumilia raia yoyote mpya ambaye atakutwa akifanya vitendo kinyume cha matakwa ya Katiba na Sheria za Nchi na kuongeza kuwa mtu huyo atakuwa amejitengeneza mazingira ya kukosa sifa za kuendelea kuwa raia wa Tanzania.

“Nasema hivi ndugu zetu hao wakitaka kuendelea kuishi hapa nchini ni lazima waishi kwa kuzingatia Katiba na Sheria za Tanzania kinyume cha hapa nilipata habari ya baadhi yao kuishi kwa kuvunja Sheria zetu nitapendekeza kwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi awanyang’ane uraia wale wote watakaobainika kutenda vitendo vya kihalifu” alisema.

Mwanri aliwataka wadau mbalimbali ikiwemo mashirika yasiyo ya kiserikali kuendelea na utoaji wa elimu ya uraia kwa Watanzania hao wapya ili waweze kuishi kulingana na utamaduni na desturi za Watanzania huku wakiweka mbele uzalendo na kwa kuzingatia umoja na mshikamano ambao uliasisiwa na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume.

Naye Meneja wa Programu kutoka Shirika lisilo la Kiserikali la Legal Services Facility (LSF), Ramadhan Masele alisema Watanzania hao wapya  wanahitaji elimu ya uraia ya kutosha ili kuwajenga uwezo wa kutambua sheria mbalimbali zinazotumika hapa nchini kwa ajili ya kuwafanya waishi kama walivyo raia wa asili ya Tanzania.

Alisema uelewa wa Katiba na Sheria mbalimbali utawasaidia kuwajengea uwezo kuishi nchini bila kupotoka na kujiingiza katika vitendo vitakavyowatia hatiani.

Kwa upande wa Mkuu wa Makazi ya Ulyankulu, Samwel Makungu alisema utoaji wa elimu ya uraia ni muhimu sana kwa raia hao wapya ili waweze kujua haki zao na mipaka ya haki zao kwa ajili ya kuwafanya kuishi vizuri nchini.

Aliongeza kuwa baadhi ya raia hao wapya wamekuwa wakikosa haki kwa sababu ya uelewa mdogo wa elimu hiyo ya uraia  na uoga kwa wengine kwa kukosa msaada wa kisheria kutoka kwa wadau mbalimbali.

Mkutano huo wa siku mbili uliandaliwa na Taasisi ya Jamii Salama Development Volunteers (JSDV) , Legal Services Facility (LSF) na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi –Kitengo cha Wakimbizi.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi