Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Warizi Kalemani Awahakikishia Wawekezaji Kutokukatika kwa Umeme
Jun 19, 2019
Na Msemaji Mkuu

 

Na. Grace Semfuko-MAELEZO

Wizara ya Nishati imewataka wawekezaji binafsi kuwekeza kwenye sekta ya viwanda ili kuongeza tija ya uzalishaji wa bidhaa kwa kuwa sasa Serikali imewekeza kwenye miundombinu ya uzalishaji wa  umeme na kwamba hautakatika tena.

Waziri wa Nishati Medard Kalemani aliyasema hayo Jijini Dar Es Salaam wakati akizungumza na Wawekezaji wenye Viwanda kuhusiana na mikakati ya Serikali ya kuongeza nishati ya Umeme kwenye gridi ya Taifa.

Waziri Kalemani alisema ni muhimu kwa wawekezaji hao kuongeza ujenzi wa viwanda kwa kuwa sasa umeme wa uhakika utakuwepo kwa asilimia kubwa kutokana na kuongeza uzalishaji wa nishati hiyo kwenye mradi mkubwa wa umeme wa Rufiji (Stiglers) utakaozalisha megawatt 2100 ambao ujenzi wake umeanza mapema mwezi huu.

“niwahakikishie wawekezaji Serikali hii inafanya mambo makubwa, hakuna kukatika katika kwa umeme tena baada ya kukamilisha miradi hii, nawaomba muanze sasa kujenga viwanda ili vitakapokamilika na umeme wa uhakika utakuwa umekamilika” alisema Kalemani

Aidha alilitaka pia Shirika la umeme Tanzania TANESCO kujipanga na kuondokana na kutokatika kwa umeme kwa mara kwa mara ili kuwapunguzia gharama za matumizi ya umeme wa mafuta wawekezaji wenye viwanda nchini.

“Shirika la umeme Tanzania TANESCO angalieni njia mbadala ya kuhakikisha umeme unakuwepo wakati wote, natumaini hamta kata kata tena umeme”alisema Kalemani.

Naye Mwenyekiti wa taaisi  ya sekta binafsi TPSF Saluma Shamte aliiomba Wizara ya Nishati kuwapa kipaumbele wawekezaji wa ndani katika ujenzi wa miradi ya umeme.

“Serikali na Wizara nawaomba hii miradi mikubwa ya uzalishaji wa umeme mngetupa sisi wawekezaji wa ndani ili kama kunahitajika wataalamu kutoka nje tutawaita sisi waje kutusaidia tu watanzania tutaweza” alisema Shamte.

Nae Mwakilishi kutoka Shirikisho la wenye viwanda Tanzania CTI Bw. Frank Daffa alisema shirikisho lake lipo tayari kufanya kazi na Serikali katika kuimarisha ujenzi wa viwanda na kuomba ushirikiano zaidi kwa manufaa ya watanzania.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi