Na Dixon Busagaga wa Globu ya Jamii,Kanda ya Kaskazini .
SERIKALI imeruhusu Wamiliki wa viwanda vya kuchakata Magogo kwa ajili ya kutengeneza Mbao kuendelea kutumia Mashine za zamani wakati wakiwa katika mchakato wa kujielekeza kwenye mabadiliko ya teknolojia .
Hatua ya serikali inatokana na ombi la Wadau wa misitu walilotoa wakati wa ziara ya siku Moja ya Naibu Waziri wa Malisili na Utalii ,Constantine Kanyasu alipotembelea Mashamba ya Miti ya North Kilimanjaro maarufu kama Rongai na West Kilimanjaro.
Mh Kanyasu pia akazungumzia suala la mgao mdogo wa Magogo kwa wachakataji huku akiahidi kuzungumza na Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) kuona namna ambavyo wadau hao watasaidika.
Meneja wa Shamba la Miti la North Kilimanjaro ,Ersnest Madata amesema changamoto iliyopo kwa sasa ni mahitaji makubwa ya mazao ya misitu katika viwanda ukilinganisha na uwezo wa Shamba hilo.
Mapema katika kikao cha Wadau wa Misitu na wafanyakazi wa mashamba ya miti ya West Kilimanjaro na North Kilimanjaro wamiliki wa viwanda vya kuchakata mazao ya misitu na wanunuzi wa mazao hayo wakapata nafasi ya kutoa kero zao kwa naibu Waziri Kanyasu.
Mashamba ya Miti ya North Kilimanjaro na West Kilimanjaro yanaukubwa Heksri 15701 yakiwa yamepakana na nchi ya Kenya, Wilaya ya Longido mkoani Arusha na Hifadhi ya taifa ya Mlima Kilimanjaro.