Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Wagonjwa 80 wa Moyo Kufanyiwa Upasuaji wa Kufungua na Bila Kufungua Kifua
Dec 08, 2017
Na Msemaji Mkuu

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na Taasisi ya Little Hearts ambao wanafadhiliwa na Taasisi ya Al- Murtada ya nchini Saudi Arabia wanatarajia kufanya matibabu ya moyo kwa wagonjwa 80  katika kambi maalum inayotarajia kuanza tarehe 10 – 14/12/2017.

Matibabu yatakayofanyika katika kambi hiyo ni ya upasuaji wa kufungua kifua na upasuaji wa bila kufungua kifua (Catheterization) kwa kutumia  mtambo wa Cathlab kwa watoto na watu wazima.

Leo tarehe 08/12/2017 madaktari bingwa wa Moyo wameanza kufanya uchunguzi kwa wagonjwa wote watakaofanyiwa upasuaji. Katika kambi  hii  ya siku tano tumepanga kufanya upasuaji wa moyo kwa wagonjwa 30 na upasuaji wa bila kufungua kifua kwa wagonjwa 50. Upasuaji wa kufungua kifua utafanyika zaidi kwa watoto na watu wazima watafanyiwa zaidi upasuaji wa bila kufungua kifua.

Kwa nama ya kipekee tunaishukuru sana Serikali kupitia Balozi wetu wa nchini Saudi Arabia Mhe. Hemedi Mgaza kwa kutoa kibali cha kuingia nchini (Visa) bila malipo kwa wataalamu wetu hawa ambao wamekuja nchini kutoa matibabu ya moyo bure kwa wagonjwa wetu.

Kama mnavyofahamu matibabu ya moyo ni ya gharama hivyo basi tunaendelea kuwahimiza wananchi  kujiunga na mfuko wa taifa wa bima ya afya ambao utawasaidia kulipa gharama za matibabu pindi  watakapougua na kuhitaji kupata matibabu.

Imetolewa na:

Kitengo cha Uhusiano na Masoko

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete

08/12/2017

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi