Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Utendaji wa JPM wawakuna wenye viwanda Mwanza
Nov 01, 2017
Na Msemaji Mkuu

Na Waandishi Wetu, Mwanza na Dar.

*Subash Patel asema Rais ameweka rekodi ya kihistoria

*Azindua viwanda vya juisi, dawa vitakavyoajiri mamia ya watu

ZIARA ya Rais John Pombe Magufuli jijini Mwanza imepokewa kwa furaha na wananchi wa mikoa ya Kanda ya Ziwa ambapo ikiwa ni miaka miwili sasa tangu aingie madarakani, uzinduzi wa viwanda na miradi mingine ya maendeleo ni ishara ya kazi kubwa iliyofanywa na Serikali yake.

Mwanzilishi na Mkurugenzi Mkuu wa Motisun Group Limited, inayomiliki viwanda mbalimbali hapa nchini kikiwemo cha jusi aina ya Sayona, Bw. Subash Patel, akiwakilisha maoni ya wawekezaji wengine walioguswa pia na utendaji wa Rais Magufuli amemweleza Rais kuwa kiongozi aliyeweka historia katika kutekeleza uanzishwaji wa viwanda nchini vingi vikiwa ndani ya kipindi kifupi.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara jana Jijini Mwanza, Bw. Patel amesema kuwa historia inaonesha Rais Magufuli ni Rais pekee ndani ya miaka miwili aliyeweza kuzindua viwanda vingi zaidi na  kuruhusu mataifa mbalimbali kuwekeza nchini.

“Kwa umri huu nilionao nimebahatika  kufanya kazi na Marais wa Awamu zote ikiwa wewe mmoja wapo. Tangu uhuru, wewe umekuwa wa kipekee uliyetambua umuhimu wa viwanda na maslahi ya wananchi kutokana na faida ya viwanda hivyo,” alisema Bw. Patel.

Aidha, Bw. Patel ameahidi kuunga mkono juhudi za Rais Dkt Magufuli za kuipeleka Tanzania katika uchumi wa kati kupitia wiwanda. Ameongeza kuwa kazi kubwa ya kampuni hiyo ni kuungana na Rais katika azma yake.

Ameongeza kuwa ifikapo mwezi Juni mwaka 2018 kampuni hiyo inatarajia kuzindua viwanda vingine vitano vitakavyozalisha bidhaa mbalimbali ikiwemo matunda, rangi za nyumba vinywaji na chuma.

Kiwanda cha vinywaji baridi cha Sayona jijini Mwanza kimejengwa kwa muda wa mwaka mmoja na nusu na kina uwezo wa kuzalisha chupa 1,200 kwa dakika moja. Tayari kiwanda hicho kimezalisha ajira za watu 200 na kinaungana na kiwanda kingine cha vinywaji baridi cha Sayona kilichopo Mboga Mkoani Pwani kusindika matunda ya wakulima na kuinua hali zao za maisha.

"Uzinduzi wa viwanda hivi ni ishara ya wazi kuwa sera za Serikali yetu ni sahihi na zinalenga kuwasaidia wananchi kupata ajira lakini na bidhaa za uhakika. Naomba watu wajue hakuna hela utaipata katika Serikali hii bure tu. Watu wawekeze kwenye viwanda kwani hata hawa wafanyabiashara wasingewekeza wasingepata hela ya Serikali.

"Sasa wale wapiga dili na mafisadi wajue wataishia jela tu hakuna fedha ya Serikali itakayoliwa kirahisi katika zama hizi. Serikali itafanyakazi na wawekezaji wote walioamua kuunga mkono sera yetu ya viwanda na tutaendelea kutatua changamoto zinazowakabili," alisema Rais.

Ndoto na dhana nzima ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. Magufuli ni Ujenzi wa Viwanda nchini ambapo mpaka sasa viwanda takribani 3306 vimefungulia ndani ya miaka miwili ya uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano.

Akiwa ziara Mwanza ambako pia amezindua kiwanda cha dawa za binadamu, daraja la waenda kwa miguu la Furahisha na viwanda vingine kadhaa, Rais Magufuli ameendelea kusisitiza juu ya ajenda yake ya kuleta mageuzi nchini.s.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi