Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Utekelezaji Mradi wa Umeme Vijijini Tabora Hauridhishi - Bodi
Oct 03, 2019
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_47491" align="aligncenter" width="750"] Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi ya Bodi ya Wakurugenzi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Styden Rwebangira (katikati), akizungumza jambo wakati Bodi hiyo ilipokutana na mkandarasi anayetekeleza mradi wa umeme vijijini mkoani Tabora (hayupo pichani). Kulia ni mjumbe wa Bodi, Luis Accarro na kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi kutoka REA, Mhandisi Jones Olotu, Oktoba 2, 2019.[/caption]

Na: Veronica Simba – Tabora

Bodi ya Wakurugenzi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), imesema hali ya utekelezaji mradi wa umeme vijijini mkoani Tabora hairidhishi.

Akitoa tathmini ya ziara waliyoifanya Oktoba 2, 2019 kukagua utekelezaji wa Mradi huo Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Kwanza mkoani humo; Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi ya Bodi husika, Mhandisi Styden Rwebangira alisema, kufuatia hali hiyo isiyoridhisha, wamelazimika kuchukua hatua ikiwemo kuzungumza kwa simu na msambazaji wa nguzo ili kazi ifanyike kwa ufanisi.

Akifafanua, alisema moja ya changamoto walizogundua ni ukosefu wa nguzo na nyaya hali inayosababisha mkandarasi kutekeleza kazi kwa kusuasua na baada ya kuzungumza na msambazaji wa nguzo ambaye ni kampuni ya Qwihaya General Enterprises, amekubali kuendelea na huduma hiyo mara moja.

“Ameahidi kuleta malori 40 ya nguzo ambayo ni sawa na takribani nguzo 4,000. Kwahiyo ni matumaini yetu kuwa kwa hapa Tabora, suala la nguzo kwa mwezi huu, tutakuwa tumetatua,” alisema Mhandisi Rwebangira.

Kuhusu suala la nyaya, alisema Bodi imemwagiza mkandarasi ahakikishe anatafuta msambazaji mwingine badala ya kumtegemea mmoja anayewahudumia kwa sasa ambaye anashindwa kutosheleza mahitaji.

[caption id="attachment_47497" align="aligncenter" width="750"] Matukio mbalimbali wakati Kamati ya Ufundi ya Bodi ya Wakurugenzi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), ilipofanya ziara kukagua utekelezaji wa mradi wa umeme vijijini mkoani Tabora, Oktoba 2, 2019.[/caption]

“Pia, tumemwagiza Mkurugenzi wa Ufundi wa REA, Mhandisi Jones Olotu, amfuatilie msambazaji huyo ili kujua tatizo ni nini na atupatie taarifa kufikia kesho.”

Awali, Mhandisi Rwebangira alieleza sababu ya msambazaji wa nguzo kusitisha huduma husika ni kucheleweshewa malipo yake ambapo alisema tayari suala hilo lilikwishafanyiwa kazi na serikali, malipo yanatolewa kwa wakati na kwamba wamemhakikishia hilo msambazaji husika ndiyo maana naye kwa upande wake akaridhia kuendelea na kazi.

Katika hatua nyingine, alieleza kuwa Bodi hiyo imegundua kuwa kumekuwa na matatizo katika kampuni za ukandarasi zinazoungana kutoa huduma ya pamoja kwa kushirikiana hususan katika masuala ya uendeshaji.

Kwa sababu hiyo, alisema kuwa wamewaagiza wakandarasi husika kujitathmini na kuhakikisha wanakuwa na lengo moja na kuwataka wasigawane kazi bali wafanye kwa pamoja kama walivyojipambanua wakati wakiomba zabuni husika.

“Tumewaonya kwamba wanapojitenga na kugawana kazi, ile nguvu na sifa iliyosababisha wakapewa zabuni husika inapotea. Wametuahidi watalifanyia kazi mara moja na kutupatia mrejesho kabla ya kukamilika kwa ziara yetu katika mikoa mingine.”

Kwa upande wake, mkandarasi husika alikiri kusuasua katika kutekeleza kazi hiyo lakini akaahidi kukamilisha kazi kwa wakati na viwango kama serikali ilivyoagiza kwani sasa wana uhakika wa kupata vifaa husika.

Katika ziara hiyo, Mhandisi Rwebangira alifuatana na mjumbe mwingine wa Bodi husika, Luis Accarro, ambao kwa pamoja wanaiwakilisha Bodi nzima na wanatarajiwa kuwasilisha ripoti ya ziara hiyo baada ya kutembelea maeneo yote yaliyopangwa ikiwemo Kigoma, Mwanza na Kilimanjaro.

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi