Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Umoja wa Mataifa Waipatia Tanzania Dola Bilioni 1.85 Kusaidia Maendeleo Nchini
Mar 25, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Na. Eva Valerian, WFM - Dodoma

Taasisi ya Umoja wa Mataifa imeipatia Tanzania msaada wa jumla ya Dola za Marekani bilioni 1.85 ambazo ni takribani shilingi  trilioni 4.3, kwa ajili ya kutekeleza afua mbalimbali katika maeneo waliyokubaliana yakiwemo sekta ya maji, afya, elimu, kilimo na jinsia na usawa kati ya shughuli za wanawake na wanaume.

Makubaliano ya msaada huu yametiwa saini Jijini Dodoma na Katibu Mkuu wa Wizara ya ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Bw. Emmanuel Tutuba, kwa niaba ya Tanzania Bara na Visiwani na Mwakilishi Mkazi wa Taasisi ya Umoja wa Mataifa, Bw. Zlatan Milisic kwa niaba ya shirika hilo.

Bw. Tutuba alisema kuwa kiwango hicho cha fedha kimeainishwa kwenye shughuli mbalimbali lakini kitakuwa ni kiwango cha kuanzia na baadae inawezekana wakati tunaendelea kutekeleza programu mbalimbali, kama patajitokeza wadau watakaoongeza miradi yao, viwango vitakuwa vina badilika na  vitaingizwa kwenye bajeti ya kila mwaka ya Wizara au Halmashauri na Mikoa husika.    

Utaratibu mpya ambao ni endelevu wa ushirikiano kati ya Taasisi za Umoja wa Mataifa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tumeona msaada huu wa fedha utaweza kutekeleza afua mbalimbali katika maeneo tuliyokubaliana, na kwa kuwa tumefanya majadiliano katika kuandaa programu hii ya miaka mitano, tutaanza kutekeleza tarehe 01 Julai 2022 mpaka tarehe 30 June 2027” Alisema Tutuba.

Aidha, Bw. Tutuba alisema katika programu hii maeneo yatakayoguswa yatachangia katika ukuaji wa uchumi, yatapunguza umasikini na kuboresha huduma mbalimbali za ustawi wa jamii. Shughuli nyingine ambazo zinaendana na vipaumbele vya Taifa vya miaka mitano kwa upande wa mpango wa tatu wa miaka mitano ya Tanzania Bara na Visiwani, kulingana na maeneo yaliyobainishwa kwenye Dira ya Maendeleo ya Zanzibar.

Kwa Upande wake, Mwakilishi Mkazi wa Taasisi ya Umoja wa Mataifa, Bw. Zlatan Milisic, alisema kuwa walifanya utafiti kwa zaidi ya mwaka mmoja na nusu na kubaini maeneo watakayoyapa kipaumbele na kutoa msaada kwa Tanzania Bara na Visiwani. Hivyo wameiomba Serikali ya Tanzania kufanya utaratibu wa kuzindua programu hii mpya ya miaka mitano ya ushirikiano.

Hafla hiyo imehudhuriwa na Kamati ya usimamizi wa ushirikiano kati ya Serikali na Mashirika ya Umoja wa Mataifa nchini, Makatibu Wakuu na Manaibu Katibu Wakuu wakiwemo Watendaji wa Serikali.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi