Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

TBS Yatoa Leseni 94 kwa Wazalishaji Wakubwa
Oct 15, 2019
Na Msemaji Mkuu

Na Neema Mtemvu SHIRIKA la Viwango Tanzania(TBS) limetoa vyeti na leseni 94 kwa wazalishaji wakubwa, wa kati na wadogo ambao bidhaa zao zimedhibitishwa na Shirika hilo kwa kukidhi matakwa ya viwango vya ubora kwa kipindi cha kuanzia Julai hadi Septemba, mwaka huu. Kati ya vyeti na leseni 94 zilizotolewa, vyeti 25 vimetolewa kwa wajasiriamali wadogo ambao bidhaa zao zimekidhi matakwa ya viwango. Akizungumza mwishoni mwa wiki wakati wa hafla ya kukabidhi vyeti na leseni hizo ,Mkurugenzi wa TBS, Dkt. Yusuf Ngenya, alisema vyeti na leseni zilizotolewa zitawasaidia wazalishaji hao kuongeza imani kwa watumiaji, kwani wanapoona alama ya ubora ya ya tbs watumiaji wanakuwa na imaani kubwa na bidhaa husika, hivyo kupanua soko. Alisisitiza kwamba bidhaa zinapokuwa zinathibitishwa ubora na shirika hilo, bidhaa hizo zikubalika moja kwa moja sokoni, zinahimili soko la ushindani na kuingia kifua mbele katika soko la nchi za Afrika Mashariki. Alisema Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Rais John Magufuli, inaendelea kuwahudumia wajasiriamali kuthibitisha ubora wa bidhaa zao bure, hivyo alitoa wito kwa wajasiriamali kujitokeza kwa wingi kuthibitisha ubora wa bidhaa zao kwa kuwa gharama zote zinalipwa na Serikali. "Natoa wito kwa wajasiriamali wote nchini kuleta bidhaa zao ili ziweze kuthibitishwa ubora wake kwani gharama zimeishalipwa na Serikali, tunashukuru Serikali kwa kutenga fungu la fedha kwa ajili ya kuwahudumia wajasiriamali," alisisitiza Dkt.Ngenya Dkt.Ngenya aliwahimiza wajasiriamali kuhakikisha wanazalisha bidhaa zenye ubora na Watanzania kuanza kupenda bidhaa za ndani ambazo zimethibitishwa ubora. "Watanzania tununue bidhaa zenye ubora kuangalia alama ya tbs hii itatufanya tuingie katika Tanzania ya viwanda kwa kupenda vya kwetu," alisema Kwa Upande wake Mwakilishi wa Mkurugenzi wa kutoka Shirika la Viwanda Vidogo (SIDO), Ridhiwani Matange, alisema kazi inayofanywa na Shirika la TBS ni nzuri inajaribu kuweka nchi katika hali ya usalama kwenye bidhaa mbalimbali. Naye Mhandisi Cdi Nyakwela kutoka Kampuni ya Plasco wazalishaji wa Makaravati ya Plastiki ,alisema vyeti hivyo walivyopatia vitawasaidia kupata soko kubwa ndani na nje ya nchi. Alisema kutokana na bidhaa hizo kuwa mpya watahakikisha wanajitangaza ili Watanzania waweze kuona kasi ya ujenzi wa Tanzania ya viwanda inavyokuja na teknolojia mpya. "TBS wametupatia leseni ya ubora ni jukumu letu sasa kuhakikisha tunazalisha makaravati ya plastiki yenye ubora na viwango kinachotakiwa na sio kufanya ujanja ujanja," alisema Mhandisi Nyakwela Mwisho..

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi