Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Tanzania na India Kuongeza Maeneo ya Ushirikiano
Jan 27, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Tanzania na India zimeahidi kuongeza maeneo mapya ya ushirikiano katika kuhakikisha maendeleo endelevu kwa maslahi mapana ya pande zote mbili.

Ahadi hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula wakati akihutubia sherehe za maadhimisho ya 73 ya Jamhuri ya India jana jioni Jijini Dar es Salaam.

Tanzania na India zimedhamiria kufanya kazi kwa karibu katika kutafuta njia bora ya kufungua fursa mpya na kuimarisha fursa mpya za biashara na uwekezaji zilizopo kati ya nchi hizo.

“Kuanza kwa safari za ndege za moja kwa moja kutoka Dar es Salaam hadi Mumbai kwa Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) na kufunguliwa kwa soko la parachichi nchini India ni miongoni mwa hatua zilizochukuliwa ili kuimarisha na kukuza uhusiano wetu katika sekta za biashara na uwekezaji pamoja na utalii kati ya India na Tanzania,” Amesema Balozi Mulamula. 

Pamoja na mambo mengine, Balozi Mulamula ameongeza kuwa Tanzania na India kwa sasa zimeanzisha ushirikiano katika usambazaji wa nishati, ujenzi wa miundombinu na kilimo.

Matarajio ya kuimarisha ushirikiano unaoendelea kati ya nchi hizi mbili ni mazuri na yanatia matumaini. 

“Uwekezaji wa India pamoja na idadi ya Wahindi wanaotembelea Tanzania kwa madhumuni ya kuwekeza katika sekta za madini, utalii, viwanda, kilimo, usindikaji wa mazao ya kilimo, nishati, usafirishaji, ujenzi, huduma za fedha na maendeleo ya rasilimali watu unaendelea kuongezeka kwa kasi,” amesema Balozi Mulamula.

Kwa upande wake, Balozi wa India nchini, Mhe. Binaya Srikanta Pradhan amesema kuwa Tanzania imekuwa na uhusiano mzuri na India ambapo uhusiano huo umekuwa ni chachu ya maendeleo kwa mataifa yote mawili na umepelekea kuongeza maeneo mapya ya ushirikiano.

“Ushirikiano na mshikamano uliopo baina ya mataifa yetu mawili umekuwa chachu ya maendeleo na lengo la ushirikiano wetu ni kukuza uchumi wetu,” amesema Balozi Pradhan 

Aidha, Balozi Pradhan amebainisha kuwa Tanzania itaendelea kuwa ya kipekee kwa taifa la India kutokana na mshikamano ambao umepelekea mataifa haya kufanya biashara, uwekezaji, kujenga uwezo, ujenzi wa miundiombinu pamoja na maendeleo ya kiuchumi.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi