Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Taarifa kwa Umma
Jan 03, 2018
Na Msemaji Mkuu

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, leo tarehe 03 Januari, 2018 ameagana na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT) anayemaliza muda wake Prof. Benno NduluIkulu Jijini Dar es Salaam.

Baada ya mazungumzo yao, Prof. Ndulu amemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa kumuamini na kufanya nae kazi tangu alipoingia madarakani na amebainisha kuwa anafurahi kumaliza kipindi chake huku uchumi wa nchi ukiwa mzuri.

Prof. Ndulu amempongeza Mhe. Rais Magufuli kwa miongozo muhimu iliyosaidia kuimarisha uchumi ikiwemo kudhibiti mfumuko wa bei ambao mwezi Novemba 2017 ulifikia asilimia 4.4 na kuongezeka kwa akiba ya fedha za kigeni kutoka Dola za Marekani Bilioni 1.8 hadi kufikia Dola za Marekani Bilioni 6 hivi sasa, hali ambayo imeimarisha uwezo wa Serikali kujiendesha na kugharamia miradi mikubwa ya maendeleo.

“Nimekuja kumuaga Mhe. Rais na kumshukuru, nafurahi kuwa naondoka wakati hali ya uchumi ikiwa nzuri, Taifa linakopesheka na kuna mazingira mazuri zaidi ya uchumi kuendelea kukua, nampongeza sana Mhe. Rais kwa kusimamia mambo mbalimbali muhimu ya kuimarisha na kukuza uchumi katika kipindi chote nilichofanya nae kazi”amesema Prof. Ndulu.

Mhe. Rais Magufuli pia amezungumza na Gavana Mteule Prof. Florens Luoga na baada ya mazungumzo hayo, Prof. Luoga amemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa uteuzi huo na kumhakikishia kuwa ataisimamia BOT ili iendelee kuwa chombo imara cha kusimamia uchumi wa nchi, kuisimamia fedha ya Tanzania na kuhakikisha nchi inatekeleza miradi mikubwa ya maendeleo kama vile ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kisasa (Standard Gauge), ujenzi wa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam na mradi wa umeme katika maporomoko ya maji ya mto Rufiji (Stiegler’s Gorge).

Prof. Luoga ameungana na Prof. Ndulu kueleza kuwa taarifa zinazotolewa na BOT kuhusu ukuaji wa uchumi zinaandaliwa kitaalamu na kwa kushirikisha vyombo mbalimbali vikiwemo Benki ya Dunia (WB) na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) na ameonya dhidi ya baadhi ya watu ambao wamekuwa wakipotosha ukweli kuhusu takwimu za uchumi zinazotolewa na BOT.

Kwa upande wake Mhe. Rais Magufuli amempongeza Prof. Ndulu kwa utumishi wake wa miaka 10 na kazi nzuri aliyoifanya kusimamia uchumi ambapo katika kipindi hicho kasi ya ukuaji wa uchumi imeongezeka kutoka wastani wa asilimia 5 hadi kufikia asilimia 7, ameimarisha usimamizi wa benki na maduka ya kubadilishia fedha, amesimamia ongezeko la akiba ya fedha za kigeni inayoiwezesha nchi kumudu kuagiza bidhaa na huduma kwa miezi 6 na kuanza kwa utekelezaji wa miradi mikubwa ya ujenzi wa reli, umeme, ununuzi wa ndege na mingine.

“Nakushukuru sana Prof. Ndulu, umefanya kazi nzuri ya kusimamia uchumi wa Taifa letu, ndio maana leo unamaliza muda wako lakini tayari Benki ya Dunia na kamisheni ya dunia inayoshughulikia teknolojia na maendeleo shirikishi wanakuhitaji ufanye nao kazi, na mimi nimeidhinisha uende ukatuwakilishe” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Mhe. Rais Magufuli amempongeza Gavana Mteule Prof. Luoga kwa kupokea uteuzi wake na amemtaka kufanya kazi ya kusimamia uchumi wa Taifa kwa ufanisi mkubwa zaidi ili nchi ipige hatua za maendeleo kwa kasi zaidi.

Wakati huo huo, Mhe. Rais Magufuli amesema mwezi ujao Serikali itatoa Shilingi Bilioni 200 kwa ajili ya kulipa madeni ya ndani yatakayokuwa yamehakikiwa yakiwemo ya wazabuni mbalimbali waliotoa huduma katika taasisi za Serikali, madai ya walimu na madai ya wakandarasi.

“Nasisitiza madeni tutakayolipa ni ya ndani, na tutalipa madeni ambayo yamehakikiwa, kwa hiyo maandalizi ya kutoa fedha hizo yaanze mara moja na ni matarajio yangu fedha hizi zitasaidia kuchochea ukuaji wa uchumi wetu” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Dar es Salaam

03 Januari, 2018

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi