Kusitishwa kwa Kongamano la Vijana Katika Kilimo
Waziri wa Kilimo Mhe. Japhet Hasunga amesitisha kongamano la vijana katika kilimo lililokuwa limepangwa kufanyika Jumanne Machi 17, 2020 katika ukumbi wa Nkrumah uliopo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Agizo hilo limetolewa leo kufuatia maelekezo yaliyotolewa na Serikali ya kuchukua tahadhari ya mikusanyiko ya watu wengi kuepusha hatari ya kusambaa kwa maambukizi ya virusi vya Corona nchini.
Wizara ya Kilimo inawataarifu wadau wote wa sekta ya kilimo na vijana waliopanga kushiriki kongamano la kujadili fursa za kilimo, mifugo na uvuvi kwa kanda ya Dar es Salaam iliyokuwa ikihusisha mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Lindi na Mtwara kusitisha kuhudhuria kongamano hilo hadi watakapotaarifiwa baadaye.
”Rais Dkt. John Pombe Magufuli ametoa rai kwa Watanzania kuchukua tahadhari na vihatarishi vinavyoweza kusababisha maambukizi ya Corona kwa kuepuka mikusanyiko ya watu wengi isiyo ya lazima” alisema Waziri Hasunga.
Mhe. Waziri Hasunga amewataka wakulima na vijana wote nchini kuendelea kuchukua hatua kwa kuzingatia maelekezo yaliyotolewa na Wizara ya Afya ili kudhibiti maambukizi ya virusi hivyo hatari vya Corona.