Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Taarifa kwa Umma
Apr 10, 2019
Na Msemaji Mkuu

USHIRIKI WA TANZANIA KATIKA MAONESHO YA KWANZA YA BIASHARA NA UCHUMI KATI YA CHINA NA AFRIKA

Dar es Salaam- Aprili 10, 2019.

Ubalozi wa Tanzania Jijini Beijing nchini China kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) inapenda kuwataarifu Jumuiya ya wafanyabiashara na wananchi wote kuwa, inaandaa ushiriki wa Tanzania katika Maonesho ya kwanza ya Biashara na Uchumi kati ya China na Afrika yatakayofanyika Mji wa Changsha, Jimbo la Hunan nchini China kuanzia tarehe 27 hadi 29 Juni, 2019.

Maonesho haya ni mkakati wa kukuza mauzo ya bidhaa za Afrika nchini China na yanabeba kauli mbiu isemayo “Win-Win Cooperation for closer China-Africa Economic and Trade Partnership” ikilenga kuleta faida za kiuchumi kwa pande zote mbili ambazo zitasaidia kuinua uchumi na biashara.

Sekta zinazohamasishwa kushiriki ni biashara, uwekezaji, fedha, kilimo, nishati, viwanda, utalii, madini na miundombinu ambazo zimekidhi viwango na ubora unaokubalika katika soko la kimataifa.

Sambamba na Maonesho hayo kutakuwa na Semina katika maeneo tofauti kama ifuatavyo;

  1. Ushirikiano na Maendeleo ya Kilimo kati ya China na Afrika
  2. Majadiliano juu ya Miundombinu na Ushirikiano wa Kifedha kati ya China na Afrika
  3. Ukuzaji wa Biashara kati ya China na Afrika
  4. Maendeleo ya Uchumi na Ushirikiano wa Biashara katika maeneo ya viwanda kwenye Halmashauri za Miji (industrial park)

Pia kutakuwa na mikutano ya kibiashara (B2B) ambapo wafanyabiashara wa China na Afrika wataweza kuingia makubaliano ili kuwa na biashara endelevu

Imetolewa na;

  Theresa Chilambo

MKUU WA KITENGO CHA MAWASILIANO

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi