Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Serikali Yapiga Marufuku Ugawaji Viwanja 'Pandikizi'
Oct 16, 2018
Na Msemaji Mkuu

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumbà na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt. Angeline Mabula amepiga marufuku ugawaji viwanja ambavyo tayari vimemilikishwa huku mmiliki wake wa awali akitafutiwa eneo lingine.

Hatua hiyo inafuatia kushamiri kwa  tabia iliyozoeleka kwa baadhi ya watendaji wa sekta ya ardhi katika halmashauri nchini kugawa maeneo ambayo tayari yana wamiliki wake wa awali na kuwapa watu wengine wenye uwezo kifedha huku wamiliki halali kuahidiwa kupatiwa kiwanja kingine.

Mhe. Mabula alitoa kauli hiyo wilayani Musoma mkoa wa Mara mwishoni mwa wiki alipokutana na watendaji wa sekta ya ardhi katika Manispaa ya Musoma pamoja na halmashauri za wilaya za Musoma na Butiama wakati wa ziara yake ya kufuatilia utekelezaji wa maagizo yake aliyoyatoa wakati wa ziara yake ya februari mwaka 2018.

"Kuanzia sasa ni marufuku kwa watendaji wa sekta ya ardhi katika halmashauri kugawa viwanja 'pandikizi' katika maeneo ambayo tayari yameshamilikishwa kwa wananchi kwani suala hili limekuwa likileta migogoro mikubwa katika sekta ya ardhi" alisema Mabula.

Kwa mujibu wa Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, suala hilo limekuwa likijitokeza sana hasa maeneo yanayovutia na mara nyingi linachangiwa na maafisa ardhi wasiokuwa waaminifu ambao humpatia mtu mwenye uwezo kiwanja kilichomilikishwa kwa ahadi ya kumpatia mmiliki halali kiwanja kingine.

Alisema,  serikali ya awamu ya tano chini ya Rais John Pombe Magufuli ambayo imekuwa ikiwatetea  watu wa hali ya chini haitavumilia hali hiyo iendelee kushamiri na kusema kuwa hatua kali zitachukuliwa kwa watendaji wote wa sekta ya ardhi watakaoendelea au kubainika kufanya mchezo huo.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi