Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Serikali Kuwekeza Zaidi Fedha Kwenye Sekta ya Kilimo na Mifugo
Aug 08, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Na. Rahma Taratibu na Hilda Mlay, SJMC, Mbeya

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Bi. Jenifa Omolo, amesema kuwa Serikali imeongeza bajeti ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2022/23 kutoka Shilingi bilioni 294 hadi Shilingi bilioni 954 ili kuwezesha sekta ya kilimo kuwa na tija kwa Taifa.

Bi. Omolo alisema hayo alipotembelea Banda la Wizara ya Fedha na Mipango pamoja na Taasisi zilizo chini yake katika Maonesho ya Nanenane yanayofanyika Kitaifa katika Uwanja wa John Mwakangale, jijini Mbeya.

Alisema kuwa lengo la kuongeza bajeti ni kuwezesha upatikanaji wa mbegu bora, kuimarisha upatikanaji wa pembejeo, utoaji wa elimu kwa wakulima kupitia kwa Maafisa Ugani, kujenga skimu za umwagiliaji pamoja na kujenga maeneo ya kuhifadhi mazao.

‘Katika bajeti hii ya 2022/2023, Serikali imewekeza fedha nyingi kuhakikisha kuwa kilimo kinatanuka na watu wanapata ajira kwa kuwa asilimia 70 ya Watanzania wanategemea kilimo ambacho ni uti wa mgongo,’ alisema Bi. Omolo.

Alisema kuwa Serikali imetenga Shilingi bilioni 361 ili kuwezekeza katika skimu za umwagiliaji ili kuwezesha wakulima kuendelea na shughuli za kilimo mwaka mzima bila kutegemea mvua za msimu na kiasi cha Shilingi bilioni 14.9 kimetengwa kwa ajili ya mafunzo kupitia kwa Maafisa Ugani ili wakulima waweze kulima kisasa.

Bi. Omolo alifafanua kuwa kuimarika kwa kilimo kutawezesha upatikanaji wa mazao ya kutosha kuwezesha nchi kujitosheleza kwa chakula ikiwa ni moja ya usalama wa nchi na pia kupatikana kwa mazao ya kuuza nje ya nchi kuwezesha nchi kupata fedha za kigeni.

Aliongeza kuwa Serikali imejipanga katika kukusanya fedha kwa mwaka 2022/23 ambapo kiasi cha Shilingi trilioni 41.4 kinatarajiwa kukusanywa huku kiasi cha Shilingi trilioni 1.2 kikitengwa kwa ajili ya sekta ya kilimo na mifugo.

Alisema Wizara ya Fedha na Mipango itashirikiana na Wizara ya Kilimo ili kuhakikisha kuwa mipango iliyopangwa na Serikali katika maeneo ya vipaumbele ili kuwezesha kukuza uchumi wa wakulima na Taifa kwa ujumla.

Bi. Omolo aliwapongeza waoneshaji katika Banda la Wizara ya Fedha na MIpango kwa kazi nzuri ya kuwaelimisha wananchi waliotembelea Banda hilo kujifunza masuala ya uchumi pamoja na huduma mbalimbali zinazotolewa na Wizara pamoja na Taasisi zake ikiwemo kujifunza elimu ya uwekezaji katika mifuko ya Serikali pamoja na mikopo inayopatikana ili waweze kukuza kilimo.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi