Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Serikali Kuendelea Kukuza Ujuzi Nchini
Jul 10, 2018
Na Msemaji Mkuu

Serikali kupitia programu ya kukuza ujuzi nchini imeendelea na majadiliano mbalimbali yatakayoiwezesha nchi kukabiliana na kiwango kidogo cha ujuzi miongoni mwa nguvukazi hususan ushiriki wa vijana katika shughuli za kiuchumi.

Hayo yamesemwa leo Jijini Dodoma na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana na Ajira Mhe. Anthony Mavunde wakati wa kikao cha majadiliano na Naibu Mawaziri wa Sekta za kipaumbele ambazo ni chachu ya ukuaji wa uchumi na maendeleo ya rasilimali watu zikiwemo za Kilimo, Nishati, Utalii, Ujenzi, TEHAMA na Usafirishaji.

Akizungumza wakati wa kikao hiko, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana na Ajira Mhe. Anthony Mavunde alieleza kuwa Programu hiyo imeleta mafanikio katika kukuza ujuzi na kuwezesha nguvukazi iliyo katika soko la ajira kuchangia katika maendeleo ya uchumi wa viwanda.

“Programu hii imekusudia kuwezesha nguvukazi ya taifa kupata ujuzi na stadi za kazi stahiki ili kumudu ushindani katika soko la ajira la ndani na nje ya nchi”, alisisitiza Mavunde.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Japhet Hasunga amesema kuwa programu hii itapelekea kuboreshwa mifumo katika sekta ya elimu na kusaidia kukuza ujuzi kwa nguvukazi kuwa watekelezaji wa vitendo.

“Ni lazima kuhakikisha vijana wanawezeshwa, vilevile kupitia programu hii wameweza kunufaika katika kuwa na uelewa wa kufanya kazi kwa vitendo na uhalisia”, alisisitiza Hasunga

Naye Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Subira Mgalu ameeleza kuwa ushirikiano wa kisekta utaleta mafanikio makubwa katika kutekeleza majukumu yao kwa pamoja na kusaidia nguvukazi nchini.

“Ni vyema vijana wakawa wanatumiwa katika miradi mbalimbali ambayo Serikali imekuwa ikianzisha nchini, kwa kufanya hivyo itasaidia vijana wengi kuchangamkia hili na kuonyesha ujuzi walio nao katika kuchangia kwenye uchumi wa nchi yao”, alisema Mgalu

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi