Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Serikali Inatambua na Kuthamini Mchango wa Taasisi za Dini Katika Kuleta Maendeleo Nchini - Simbachawene
Oct 01, 2023
Serikali Inatambua na Kuthamini Mchango wa Taasisi za Dini Katika Kuleta Maendeleo Nchini - Simbachawene
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene akizungumza kwenye hafla ya chakula cha hisani iliyoandaliwa kwa ajili ya kuchangia ukamilishaji wa ujenzi wa jumla wa Kanisa Katoliki la Parokia ya Utatu Mtakatifu Changanyikeni jijini Dar es Salaam.
Na Lusungu Helela - DSM

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan inathamini na kutambua mchango mkubwa wa taasisi za dini katika shughuli mbalimbali za maendeleo hususani katika kuimarisha amani na utulivu wa nchi. 

 

Mhe. Simbachawene ametoa kauli hiyo alipokuwa akimwakilisha Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Mpango kwenye hafla ya chakula cha hisani iliyoandaliwa kwa ajili ya kuchangia ukamilishaji wa ujenzi wa jumla wa Kanisa Katoliki la Parokia ya Utatu Mtakatifu Changanyikeni jijini Dar es Salaam.

 

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Simbachawene amewapongeza wanaparokia hao kwa hatua kubwa waliyofikia katika ujenzi wa kanisa hilo huku akiwasihi kuendelea kuiunga mkono Serikali katika masuala ya maendeleo.

 

"Hongereni sana kwa hatua hii kubwa mliyofikia ya umaliziaji wa Kanisa hili, hakika mmefanya kazi kubwa na nzuri", amesema Mhe. Simbachawene.

 

Aidha, Mhe. Simbachawene amewapongeza wanaparokia hao kwa kuwa na mpango kazi makini wa ukamilishaji wa kanisa hilo ambapo wanatarajia ifikapo tarehe 7 Januari, 2024 litatabarikiwa na Askofu Mkuu wa Jimbo kuu Katoliki la Dar es Salaam, Yuda Thaddeus Ruwa’ichi.

 

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Parokia ya Kanisa hilo, Gallen Mvungi amesema jumla ya kiasi cha shilingi milioni 250 kinahitajika kukamilisha ujenzi wote ambapo shilingi milioni 50 tayari zimeshakusanywa na wanaparokia hiyo.

 

Katika hafla hiyo, jumla ya kiasi cha shilingi milioni 110 zilikusanywa huku kiasi cha shilingi milioni 78 zikiwa ni ahadi na shilingi milioni 32, fedha taslimu.

 

Hafla hiyo ilitanguliwa na misa maalum ilyoongozwa na Mwakilishi wa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Askofu Msaidizi Vicent Mpwaji na kuhudhuriwa pia na viongozi mbalimbali akiwemo Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania, Bw. Masanja Kadogosa.


 


 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi