Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

RC Wangabo Awaonya Wanarukwa Kutokuwa Chanzo cha Mauaji
Jan 22, 2020
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_50308" align="aligncenter" width="750"] Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo akizungumza na wananchi wa kijiji cha Mkwamba kilichopo Wilaya ya Nkasi katika ziara yake ya kuelimisha na kuwakataza wananchi kuacha tabia ya kuharibu vyanzo vya maji kwa kufanya shughuli za kibinadamu katika milima ya safu za Lyamba Lyamfipa mkoani Rukwa.[/caption]

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo amewaonya wananchi wanaokaa karibu na milima ya Lyamba Lyamfipa kuacha maramoja kufanya shughuli za kibinaadamu katika milima hiyo baada ya shughuli hizo kuharibu mazingira na vyanzo vya maji vilivyomo na matokeo yake kuwasababishia maisha magumu wananchi wanaoishi katika bonde la ziwa Rukwa lililozungukwa na milima hiyo.

Amesema kuwa kuwa na maji ni jambo zuri lakini kuendelea kubaki nayo kwa miongo kadhaa ijayo ni jambo kubwa zaidi na kuongeza kuwa milima hiyo ndio chanzo cha maji cha Ziwa Rukwa, ziwa lililobeba jina la mkoa na hivyo kutokuwepo kwa ziwa hilo ni kuondoa asili ya mkoa jambo ambalo hataruhusu litokee.

“Milima hii yote ndio chanzo cha maji cha watu wanaoishi bonde la Ziwa Rukwa pamoja na Ziwa Rukwa lenyewe, mkiharibu hiyo milima hiyo ni sawa na kufanya mauaji kwa watu wanaoishi katika bonde la Ziwa Rukwa, kwasababu watakosa maji wale wananchi lakini hata mifugo itakosa maji huko lakini tatu hata ziwa rukwa lenyewe litakauka litajaa tope kwa hivyo vitendo vya kibinaadamu vya kukata miti na maji yaliyopo yatakwisha litafutika,” Alisisitiza

Mh. Wangabo ameyasema hayo alipofanya ziara katika vijiji vilivyo karibu na milima ya Safu za Lyamba Lyamfipa katika Wilaya ya Nkasi na Sumbawanga na kuendelea kutoa elimu kwa wananchi hao juu ya utunzaji wa vyanzo vya maji na milima hiyo ili kupunguza athari za mvua zinazowatokea watu wanaoishi katika bonde la Ziwa Rukwa.

Amesema kuwa kutotunza vyanzo vya maji na vyanzo vya mvua kutasababisha kilimo chetu kutokuwa na tija na kueleza kuwa milima hiyo ndio tegemezo kwa mkoa wa Rukwa pamoja na mikoa ya jirani na hivyo utunzaji wake ni umuhimu kwa nchi.

Ameongeza kuwa mahala ambapo pamefyekwa na kulimwa si sawa na mahali ambapo hapajalimwa na penye miti kwani mvua ikija itachimba mahali ambapo pameshaharibika na kuacha maeneo ambayo yana miti na nyasi.

Katika hatua nyingine amewataka wananchi hao kuwa watulivu na kutoshawishiwa na wanasiasa wasiopenda utulivu uliopo hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu wa Madiwani, Wabunge na Rais.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi