Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Rais Mhe. Dkt. Magufuli Amtaka Prof. Mbarawa Kuwachukulia Hatua Wanaochelewesha Miradi ya Maji
Oct 17, 2019
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_48150" align="aligncenter" width="750"] Rais Dkt. Magufuli Akiongea na Wananchi Wilayani Masasi Mkoani Mtwara[/caption]

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amemtaka Waziri wa Maji Prof. Makame Mbarawa kuchukua hatua dhidi ya wataalamu wa wizara hiyo wanaochelewesha utekelezaji wa miradi ya maji licha ya Serikali kutoa fedha za miradi hiyo.

Mhe. Rais Magufuli ametoa agizo hilo leo tarehe 16 Oktoba, 2019 alipokuwa akizungumza na wananchi wa Masasi Mkoani Mtwara baada ya Mkurugenzi wa Maji Bw. Nuntufye Mwamsojo kueleza kuwa ujenzi wa chujio ya maji kwa ajili ya mji huo unasuburi kufanyika kwa upembuzi yakinifu uliopangwa kuchukua muda wa miezi 6.

Mhe. Rais Magufuli aliyechukizwa na mipango ya ucheleweshaji miradi amesema wataalamu wa Wizara ya Maji hawana sababu za msingi za kutumia muda mrefu kufanya upembuzi yakinifu wakati wananchi wana tatizo la maji na hivyo ametoa wiki mbili kwa upembuzi huo kukamilika na ujenzi wachujio kuanza mara moja.

“Waziri Mbarawa unafanya kazi nzuri sana, lakini nataka uwe mkali, hawa wataalamu wako wa maji wizarani wanakuangusha, nenda ukawashughulikie hata kama ni kuwafukuza wafukuze, wananchi hawawezi kuendelea kukosa maji halafu wataalamu wanaleta lugha za upembuzi yakinifu miezi 6 kwa ajili ya chujio ya maji?” amehoji Mhe. Rais Magufuli.

Akiwa njiani kutoka Ruangwa kwenda Lindi Mjini kupitia Masasi Mkoani Mtwara Mhe. Rais Magufuli amesimama na kuzungumza na wananchi wa Ikungu, Nachingwea, Naipanga, Lukuledi, Chigugu na Ndanda ambapo amewahakikishia kuwa Serikali itawalipa wakulima wa korosho ambao hawajalipwa fedha zao kuanzia Jumanne ijayo tarehe 22 Oktoba, 2019.

Naibu Waziri wa Kilimo Mhe. Hussein Bashe amesema maandalizi ya kuwalipa wakulima hao yamekamilika ambapo shilingi Bilioni 53.6 zimeandaliwa kumaliza madeni ya wakulima wa korosho yaliyobaki na pia amebainisha kuwa Serikali imeanza kuchukua hatua dhidi ya viongozi wa vyama vya ushirika waliowaibia wakulima ili wafikishwe katika vyombo vya kisheria.

Mjini Nachingwea Mhe. Rais. Magufuli amelazimika kukagua eneo linapojengwa soko na eneo kilipohamishwa kituo cha mabasi baada ya wananchi wa Mji huo kuwalalamikia viongozi wa Wilaya kuwa wameshindwa kukamilisha miradi hiyo licha ya Serikali kutoa fedha.

Baada ya ukaguzi huo, Mhe. Rais Magufuli amewaonya Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea Bi. Rukia Muwango na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea Bw. Bakari Mohammed Bakari kutokana na kutotekeleza majukumu yao ipasavyo na amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Lindi Bw. Godfrey Zambi kufuatilia maagizo anayoyatoa kwa viongozi wa Mkoa huo.

Akiwa katika Kijiji cha Chigugu Wilayani Masasi, Mhe. Rais Magufuli amemuagiza Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Brig. Jen. John Mbungo kumuondoa Kamanda wa TAKUKURU Mkoani wa Mtwara Bw. Steven Mafipa na kufanya uteuzi mwingine wa Kamanda wa TAKUKURU wa Mkoa huo kutokana na kushindwa kuwashughulikia viongozi wawili wa chama cha msingi cha ushirika (AMCOS) wanaodaiwa kuwaibia fedha wakulima wa korosho wa Chigugu.

Mhe. Rais Magufuli amemuagiza Brig. Jen. Mbungo kufanya uteuzi huo leo ili kesho tarehe 17 Oktoba, 2019 mteule huyo aripoti katika kituo chake cha kazi na kwenda moja kwa moja kushughulikia malalamiko ya wakulima wanaodai kuibiwa fedha na viongozi wa vyama vya msingi vya ushirika.

Mhe. Rais Magufuli amempa siku 5 Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mtwara Blasius Chatanda kuwakamata watuhumiwa Salum Chilundu na Juma Mpopo ambao wametanjwa na Diwani wa Kata ya Chigugu Mhe. Amina Mpandula kuwa wamehusika katika wizi wa fedha za wakulima wa korosho kupitia AMCOS.

Akiwa Ndanda, Mhe. Rais Magufuli amepokea maombi ya wanafunzi wa shule kongwe ya sekondari ya Ndanda ambao wameomba Serikali isaidie kukarabati miundombinu ya shule hiyo na kujenga bwalo la chakula ambapo ameagiza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kutoa shilingi Milioni 100 kwa ajili hiyo.

Halikadhalika, Mhe. Rais Magufuli amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Mhe. Gelasius Byakanwa na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile kubaki Ndanda ili kufuatilia madai ya wananchi waliolalamikia kutozwa fedha nyingi za matibabu wanapokwenda kutibiwa katika Hospitali ya Ndanda ambayo ni Hospitali Teule ya Wilaya ya Masasi (DDH) na ameonya kuwa endapo itathibitika kuwa madai ya wananchi ni kweli Serikali itajenga hospitali ya Serikali itakayoweza kutoa huduma kwa gharama nafuu.

Mhe. Rais Magufuli pia ameahidi kuwa Serikali itatoa shilingi Milioni 100 kwa ajili ya upanuzi wa zahanati ya Naipanga, ametoa shilingi Milioni 10 kwa shule ya Lukuledi Maalum (ambayo ina wanafunzi viziwi) kwa ajili ya kutatua changamoto za shule hiyo likiwemo tatizo la maji na amechangia shilingi Milioni 9 kwa shule za Sekondari Mbemba na Sekondari Isdor Shirima na Shule ya Msingi Chigugu.

Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Lindi

16 Oktoba, 2019

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi