Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Rais Magufuli Aahidi Tani 700,000 za Chakula kwa Zimbabwe
May 29, 2019
Na Msemaji Mkuu

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amesema Tanzania itaiuzia Zimbabwe tani 700,000 za mahindi kufuatia nchi hiyo kukabiliwa na upungufu wa chakula.

Mhe. Rais Magufuli ametoa ahadi hiyo leo muda mfupi baada ya kufanya mazungumzo rasmi kati yake na Rais wa Jamhuri ya Zimbabwe, Mhe. Emmerson Mnangagwa yaliyofanyika Ikulu Jijini Harare.

Ameeleza kuwa katika msimu uliopita Tanzania ilipata ziada ya chakula ya tani Milioni 3.3 baada ya kuvuna tani Milioni 16.8 ambapo kati yake mahitaji ya nchi ni tani Milioni 13.5.

Katika mazungumzo hayo, Mhe. Rais Magufuli ameikaribisha Zimbabwe kujifunza jinsi Tanzania inavyotoa mafunzo ya kujenga Taifa kwa vijana kupitia Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na amebainisha kuwa JKT inasaidia vijana kuwa wazalendo wa kweli, kuwa na nidhamu na wakakamavu.

Mhe. Rais Magufuli pia ameelezea kutofurahishwa kwake na kutofanyika kwa Kamati ya Kudumu ya Pamoja (Joint Permanent Commission – JPC) tangu mwaka 1998 hali iliyosababisha kukosekana kwa msukumo wa kutosha wa kutekeleza maeneo muhimu ya uhusiano yenye kuimarisha uchumi wa pande zote na hivyo ametaka Mawaziri na Wataalamu kufanya kikao cha JPC ndani ya mwezi mmoja.

Aidha, Mhe. Rais Magufuli amesisitiza kuwa Tanzania itaendelea kuwa rafiki wa kweli wa Zimbabwe na ameahidi kuwa tayari kuwaleta walimu watakaofundisha lugha ya Kiswahili katika shule na vyuo vya Zimbabwe.

Halikadhalika, Mhe. Rais Magufuli ametoa wito kwa wafanyabiashara na wawekezaji wa Tanzania na Zimbabwe kuongeza biashara kati ya nchi hizo ikilinganishwa na hali ilivyo hivi sasa ambapo kiwango cha biashara katika nchi hizo ni shilingi Bilioni 22.578 tu.

Kwa upande wake, Mhe. Rais Mnangagwa amemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa utayari wake wa kutoa mahindi kwa ajili ya kusaidia upungufu wa chakula nchini Zimbabwe na amesisitiza kuwa Wazimbabwe watafurahi kupata chakula kutoka kwa ndugu zao Watanzania.

Kuhusu maeneo mengine ya ushirikiano ambayo Mawaziri walijadiliana kabla ya mazungumzo hayo, Mhe. Rais Mnangagwa amesema Zimbabwe ipo tayari kuyatekeleza na kukamilisha maeneo mapya yatakayokubalika na kutiwa saini makubaliano yake.

Baadhi ya maeneo hayo ni pamoja na Zimbabwe kuitumia bandari ya Mtwara katika kusafirisha mizigo yake, kushirikiana katika utalii na usafiri wa anga, kubadilishana utaalamu katika kilimo, mifugo na uvuvi.

Baada ya mazungumzo hayo viongozi hao wamekutana na Waandishi wa Habari na kuwaeleza juu ya yaliyojiri wakati wa mazungumzo.

Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Harare

29 Mei, 2019

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi