Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Rais Dkt. Magufuli Awaongoza Watanzania Kuipokea Ndege aina ya Airbus A220-300
Dec 23, 2018
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_39207" align="aligncenter" width="750"] Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akikata utepe pamoja na Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa,Balozi wa Canada Pamela O’donnel pamoja na viongozi wengine mara baada ya kuwasili kwa Ndege mpya aina ya Airbus 220-300 ambayo imenunuliwa na Serikali.Hafla iliyofanyika katika Uwanja ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Desemba 23,2018

[/caption] [caption id="attachment_39204" align="aligncenter" width="750"] Katibu mkuu kiongozi Balozi Dkt.John Kijazi pamoja na katibu mkuu wa Wizara ya Ujenzi mawasiliano na Uchukuzi Dkt.Leonard Chamuriho wakisaini mkataba wa makabidhiano ya Ndege mpya ya Airbus 220-300 itakayokabidhiwa katika shirika la ndege la Tanzania mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli,Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa pamoja na viongozi wengine wakishuhudia kabla ya kuwasili kwa Ndege mpya aina ya Airbus 220 - 300 ambayo imenunuliwa na Serikali.Hafla iliyofanyika katika Uwanja ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Desemba 23,2018[/caption]

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 23 Desemba, 2018 amewaongoza Watanzania kuipokea ndege mpya aina ya Airbus A220-300 iliyonunuliwa na Serikali kwa lengo la kuimarisha huduma za usafiri wa anga kupitia Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL).

Ndege hiyo (A220-300) ni kati ya ndege 2 za aina hiyo zilizonunuliwa na Serikali ya Tanzania kwa kutumia fedha za ndani na ndege ya pili inatarajiwa kuwasili hapa nchini wiki 2 zijazo kutoka nchini Canada ambako zinatengenezwa.

Sherehe ya mapokezi ya ndege hiyo imefanyika katika kituo namba 1 (terminal one) cha Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Mke wa Rais Mhe. Mama Janeth Magufuli, Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, Spika wa Bunge Mhe. Job Yustino Ndugai, Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, Mawaziri na Naibu Mawaziri, Balozi wa Canada hapa nchini Mhe. Pamela O’Donnel, Wabunge, Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu, viongozi wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, viongozi wakuu wa taasisi za umma na binafsi, viongozi wa Dini, viongozi wa vyama vya siasa na viongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Paul Makonda.

[caption id="attachment_39193" align="aligncenter" width="750"] Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akimpongeza mmoja wa Marubani Kapteni Pandya aliyekuja na ndege hiyo mara baada ya kuwasili katika katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.[/caption]

Kuwasili kwa ndege hiyo (A220-300) kunafanya jumla ya ndege zilizowasili nchini tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani kufikia 5 kati ya ndege 7 zilizonunuliwa.

Akizungumza na Watanzania muda mfupi kabla ya ndege hiyo kuwasili, Mhe. Rais Magufuli amesema Serikali inatekeleza kwa vitendo Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2015 ambayo inaelekeza kuimarishwa kwa usafiri wa anga na ameagiza kununuliwa kwa ndege ya 8 aina ya Bombardier Dash 8-Q400 ili kutimiza lengo la mpango wa Maendeleo wa ATCL la kufikia ndege 8 ifikapo mwaka 2021/22.

Mhe. Rais Magufuli amewapongeza Watanzania wote, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, ATCL, Wabunge na wadau wengine wote kwa mafanikio ya kununua ndege hiyo na ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kulipa kodi ili Serikali iweze kutekeleza mipango mingine mingi ya kuliendeleza Taifa.

Amefafanua kuwa kutokana na kodi Serikali imeweza kununua ndege, kujenga barabara nyingi na nyingine zinaendelea kujengwa, kujenga njia mpya ya reli ya kati na kufufua reli za zamani, kujenga meli mpya na kukarabati meli za zamani, kupanua viwanja vya ndege vya kimataifa vya Dar es Salaam (JNIA) na Kilimanjaro (KIA), kukarabati viwanja vya 11 nchini na kupanua bandari.

[caption id="attachment_39205" align="aligncenter" width="750"] Ndege mpya aina ya Airbus 220-300 ambayo imenunuliwa na Serikali ikimwagiwa maji ikiwa ni ishara ya karibu na heshima (Water salute) kwa mara ya kwanza katika ardhi ya Tanzania Uwanja ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Desemba 23,2018[/caption] [caption id="attachment_39203" align="aligncenter" width="750"] Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akiwa ndani ya ndege na Mkewe Janeth Magufuli ,Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa,Spika wa Bunge Job Ndugai,Balozi wa Canada Pamela O’donnel ,Katibu mkuu kiongozi Balozi Dkt.John Kijazi pamoja na viongozi wengine mara baada ya kuwasili kwa Ndege mpya aina ya Airbus 220-300 ambayo imenunuliwa na Serikali.Hafla iliyofanyika katika Uwanja ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Desemba 23,2018[/caption]

Pamoja na kuipongeza ATCL kwa kuzalisha faida ya shilingi Bilioni 28 tangu ianze kupatiwa ndege mpya na Serikali Oktoba 2016, Mhe. Rais Magufuli amelitaka shirika hilo kuhakikisha linazalisha faida na kushughulikia mapungufu yaliyoanza kujitokeza ikiwemo hujuma katika ukatishaji wa tiketi.

Aidha Mhe. Rais Magufuli ameagiza viongozi na wafanyakazi wa Serikali ambao waliwahi kukatiwa tiketi kwa kulipiwa na Serikali na hawakusafiri, kurejesha Serikalini fedha hizo mara moja na ametaka apewe orodha ya viongozi na wafanyakazi hao (wanaokadiriwa kuwa takribani 100).

Halikadharika Mhe. Rais Magufuli amesema Serikali inaendelea kuimarisha Chuo cha Usafirishaji (NIT) ikiwemo kukinunulia ndege 5 kwa ajili ya mafunzo kwa marubani na wahandisi, ikiwa ni juhudi za kuhakikisha nchi inakuwa na marubani na wahandisi wa kutosha pamoja na kujenga uwezo wa kufanya matengenezo ya ndege hapa hapa nchini kupitia karakana ya ndege iliyopo KIA.

Wakati huo huo, Mhe. Rais Magufuli ametoa shilingi Milioni 10 kwa Kepteni Mstaafu Narzis Peter Mapunda aliyekuwa rubani wa kwanza wa ndege za ATC na ambaye wakati wa kuvunjika kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki alionesha uzalendo mkubwa wa kuirejesha hapa Tanzania moja ya ndege za shirika la ndege la Afrika Mashariki baada ya kutolewa amri kuwa Ndege zote ziegeshwe Nairobi nchini Kenya.

[caption id="attachment_39200" align="aligncenter" width="750"] Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akiwapungia mkono wa kuwaaga Wananchi na wanachama wa CCM waliojitokeza katika mapokezi ya Ndege mpya aina ya Airbus 220-300 ambayo imenunuliwa na Serikali.Hafla iliyofanyika katika Uwanja ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Desemba 23,2018[/caption]

Pamoja na kutoa fedha hizo Mhe. Rais Magufuli ameiagiza ATCL kumsafirisha bure Kepteni Mstaafu Mapunda pamoja na Mkewe mahali popote watakapohitaji kusafiri kwa ndege za ATCL ikiwa ni kutambua mchango wake mkubwa kwa Taifa na uzalendo aliouonesha bila kujali kama kitendo chake cha kuirejesha ndege hiyo nyumbani Tanzania kingeweza kugharimu maisha yake.

“Naomba kutoa wito kwa Watanzania hasa vijana, tuwe wazalendo kama alivyokuwa Kepteni Mapunda, yeye aliposikia Jumuiya ya Afrika Mashariki imevunjika na kuna agizo ndege zote wazipaki Nairobi Kenya, alijifanya kama anakwenda kupaki badala yake akairusha na kuja nayo moja kwa moja Tanzania, hakujali kutunguliwa ama kukosa mawasiliano ya waongoza ndege, tunakushukuru sana Mzee Mapunda” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Mapema akitoa taarifa ya maendeleo ya ATCL tangu Serikali ikodishe ndege kwa shirika hilo, Katibu Mkuu wa Uchukuzi Dkt. Leonard Chamriho amesema hadi Oktoba 2018 ATCL ilikuwa imelipa Serikalini shilingi Bilioni 6.7 ikiwa ni gharama za ukodishaji wa ndege, imelipa kodi ya shilingi Bilioni 8.6, imeongeza idadi ya abiria waliosafirishwa kutoka 5,600 hadi 34,000, imeongeza umiliki wa soko la ndani kutoka asilimia 2.5 hadi 36 na kuongeza kiwango cha kuruka na kutua kwa wakati kutoka asilimia 22 hadi 87.

Pia Dkt. Chamriho amesema idadi ya marubani imeongezeka kutoka 11 hadi kufikia 50 wengi wao wakiwa ni Watanzania waliofundishwa hapa nchini na nje ya nchi, imeongeza wahandisi na mafundi kutoka 31 hadi kufikia 87 wakiwemo wahandisi wazawa 36 na mafundi 45.

Spika wa Bunge Mhe. Job Yustino Ndugai na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma wameipongeza Serikali kwa mafanikio makubwa ya kununua ndege na kuimarisha ATCL na wametoa wito kwa wafanyakazi wa ATCL kuhakikisha shirika hilo halirudi katika historia mbaya ya kufirisika.

Nae Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe amesema wizara hiyo imejipanga kuhakikisha ATCL inajiimarisha kwa huduma na ufanisi, na kuhakikisha karakana iliyopo KIA inafufuliwa ili kuondokana na gharama kubwa ya matengenezo ya ndege yanalazimu kuzipeleka ndege nchini Canada.

Katika sherehe hizo Mhe. Rais Magufuli ameshuhudia tukio la kutia saini makubaliano ya kukodisha ndege kwa ATCL ambapo Katibu Mkuu Kiongozi Mhe. Balozi John Kijazi ametia saini na kukabidhi kwa niaba ya Serikali.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi