Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Nitaanza kwa Kushughulikia Tatizo la Mimba Mashuleni -Naibu Waziri George Kakunda
Oct 18, 2017
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_20374" align="aligncenter" width="750"] Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. George Kakunda akisisitiza jambo alipotembelea Makao Makuu ya Chama cha Walimu Tanzania (CWT) jana jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Katibu Mkuu wa Chama hicho Bw. Yahya Msulwa. Naibu Waziri Kakunda ametembelea baadhi ya wadau na kujadiliana kuhusu mbinu za kudhibiti mimba kwa watoto wa kike shuleni.[/caption]

Na: Thobias Robert

Naibu Waziri ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) anayeshughulikia elimu George Kakunda amesema kuwa ataanza kutekeleza majukumu yake kwa kushughulikia tatizo la mimba mashuleni.

Akizungumza kwa nyakati tofauti wakati wa ziara yake kutembelea Chama cha Walimu, Idara ya Mahakama na Jeshi la Polisi nchini jana, Naibu Waziri alieleza kuwa tatizo la mimba kwa watoto wa kike mashuleni limekuwa kubwa na kuathiri sio tu maendeleo yao bali taifa kwa jumla.

‘’Tatizo hili ni kubwa na athari zake si kwa wasichana tu wanaolazimika kuacha shule na kupoteza fursa ya kuendelea na masomo bali hata kwa taifa kwa kuwa linatunyima wasomi na wataalamu wa kuendeleza nchi yetu”Alisema Naibu Waziri.

[caption id="attachment_20377" align="aligncenter" width="750"] Jaji Kiongozi wa mahakama kuu nchini, Jaji Ferdinand Wambali akimueleza jambo Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) George Kakunda ofisi kwake wakati wa ziara ya Naibu Waziri huyo jana jijini Dar es Salaam. Naibu Waziri Kakunda ametembelea baadhi ya wadau na kujadiliana kuhusu mbinu za kudhibiti mimba kwa watoto wa kike shuleni.[/caption]

Alibainisha kuwa mwaka 2012 wasichana takriban 2,400 kwa shule za msingi pekee walipata ujauzito ingawa idadi hiyo alieleza kuwa imekuwa ikipungua ambapo mwaka jana wasichana 250 wameripotiwa kupata ujauzito. Hata hivyo, alieleza kuwa tatizo hilo linaonekana kuwa kubwa zaidi kwa upande wa Sekondari.

Naibu Waziri alieleza kuwa kuongezeka kwa tatizo la mimba kwa wasichana mashuleni kunachangiwa na kuporomoka kwa maadili katika jamiii, baadhi ya mila na desturi, kuongezeka kwa matumizi ya simu za kisasa (smartphone) na vishawishi vingine.

Aidha, alibainisha kuwepo kwa ukiukwaji mkubwa wa sheria unaofanywa na Mahakama, Jeshi la Polisi pamoja na Chama cha Walimu kwa kuwateteta baadhi ya watumishi wanaohusika na vitendo vya kuwapa mimba wasichana hivyo kutoa wito wa watumishi kuacha mara moja mwenendo huo na kutaka sheria zifuatwe ipasavyo.

[caption id="attachment_20380" align="aligncenter" width="750"] Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu nchini, Jaji Ferdinand Wambali (Kushoto) akiagana na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) George Kakunda baada ya ziara ya Naibu Waziri huyo jana jijini Dar es Salaam. Naibu Waziri Kakunda ametembelea baadhi ya wadau na kujadiliana kuhusu mbinu za kudhibiti mimba kwa watoto wa kike shuleni.[/caption]

“Mwaka jana bunge lilipitisha sheria kali kwa mtu yeyote atakayempa mimba mwanafunzi wa kike, anatakiwa kupewa adhabu ya kufungwa jela miaka 30, mtu yeyote anayemkatisha masomo mtoto wa kike, yaani anayemuozesha, anayewezesha, anayeshabikia, anayefungisha ndoa wakiwemo wazazi Masheikh, Mapadre ama walezi nao pia wanapaswa kufungwa miaka 30,” alisisitiza Naibu Waziri Kakunda.

Aidha alisema kuwa mahakama, polisi pamoja na wazazi wamekuwa hawalichukulii kwa uzito suala hili kwani rushwa ndogo ndogo hususani ngazi za halmashauri bado zimeendelea kuongeza ukubwa wa tatizo hilo hivyo ametoa wito kwa mahakama pamoja na polisi kulivalia njuga jambo hilo ili kuwanusuru na kuwaokoa watoto wa kike dhidi ya janga la kupata mimba hapa nchini.

[caption id="attachment_20381" align="aligncenter" width="750"] Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu (CWT) Bw. Yahya Msulwa akifafanua jambo kwa Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) George Kakunda kufuatia ziara aliyoifanya Naibu Waziri huyo katika Makao Makuu ya Chama hicho jana jijini Dar es Salaam. Naibu Waziri Kakunda ametembelea baadhi ya wadau na kujadiliana kuhusu mbinu za kudhibiti mimba kwa watoto wa kike shuleni.[/caption] [caption id="attachment_20382" align="aligncenter" width="750"] Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) George Kakunda akimsikiliza Msaidizi wa IGP Kamishna Mussa Ali Mussa ofisini kwake katika ziara aliyoifanya Makao Makuu ya Jeshi la Polisi jana jijini Dar es Salaam ili kujadili namna ya kudhibiti tatizo la mimba kwa watoto wa kike mashuleni. (Picha na: Thobias Robert)[/caption]

“Kuna baadhi ya watendaji wa vijiji, kata, walimu wakuu waliopo chini ya halmashauri wamekuwa wakipatanisha kesi hizi nje ya utaratibu, mfano mkosaji anaweza kulipishwa ng’ombe, fedha au hata mbuzi kesi inaisha hivyo tu, kwa hiyo nikuombe Jaji kiongozi upeleke msukumo mkubwa kwa watumishi wa mahakama na Jeshi la Polisi katika ngazi za halmashauri ili waweze kulishughulikia suala hili kwa mujibu wa sheria,” alisistiza Naibu Waziri Kakunda.

Kwa upande wake Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu Ferdinand Wambali alisema kuwa mahakama inatambua kuna changamoto katika utekelezaji wa sheria hususani mazingira ya kutungwa kwa sheria hiyo, utekelezaji wake lakini pia ushirikiano kutoka kwa wananchi.

“Sheria nyingi zinatungwa lakini wananchi wengi haziwafikii katika hali ya kawaida, hivyo unaweza kuona kuwa makosa yanaendelea ni kwa sababu wananchi hawajaelewa haswa nini kinachopaswa kufanywa, lakini pia wananchi hawaelewi hata namna ya kutoa ushirikiano kwa kutoa ushahidi kwa baadhi ya makosa ya jinai kwa polisi na mahakama,” alisema Jaji Wambali.

Kwa upande wake, Msaidizi wa IGP Simon Sirro, Kamishna Mussa Ali Mussa kutoka makao makuu ya polisi, alisema kuwa tatizo hilo linafanyiwa kazi kwa ukaribu zaidi na polisi kwa kushirikiana na jamii ambapo mpaka sasa baadhi ya mambo wameshayafanya ikiwemo kuanzisha dawati la jinsia kwa vituo vya polisi katika halmashauri mbalimbali kwa lengo la kukabiliana na changamoto hizo.

“Katika mfumo wa ushirikishwaji tulionao, tumeteua askari mmoja kwa kila kata ili huyu askari akashirikiane na kamati ya ulinzi ya kata kutatua kero mbalimbali zilizopo ndani ya kata ikiwemo watoto wa kike kupata ujauzito wakiwa shuleni,” alieleza Kamishna Mussa.s

Naibu Waziri Kakunda ambaye aliteuliwa hivi karibuni alifanya ziara hiyo ili kushauriana namna bora ya ushirikiano kati ya wizara yake na taasisi hizo kupunguza kama si kutokomeza kabisa tatizo mimba za wasichana mashuleni.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi