Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

NEC:   Uchaguzi  Mdogo  wa  Majimbo  Mawili  na  Kata  Nne  Kufanyika Feb, 17, 2018.
Jan 03, 2018
Na Msemaji Mkuu

 

Subira  Kaswaga - NEC

Uchaguzi  Mdogo  wa  majimbo  ya  Siha mkoani  Kilimanjaro  na  Kinondoni mkoani  Dar  es  Salaam pamoja  na  Kata  nne  za  Tanzania  Bara  utafanyika  tarehe  17/02/2018, kufutia waliokuwa Wabunge katika majimbo hayo kujivua Uanachama na kukosa sifa za kuendelea kuwa wabunge.

Taarifa ya Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Jaji Mkuu Mstaafu wa Zanzibar Hamid Mahmod Hamid imeeleza kuwa pamoja na Majimbo hayo,pia Kata nne za Isamilo    katika  Halmashauri  ya Wilaya  ya  Nyamagana mkoani  Mwanza,  Manzase  Halmashauri  ya  Wilaya  ya Chamwino  mkoani  Dodoma, Madanga  Halmashauri  ya   Wilaya  ya  Pangani  mkoani  Tanga  na  Kimagai  Halmashauri  ya  Wilaya  ya  Mpwapwa  mkoani  Dodoma zitafanya Uchaguzi mdogo

Aidha, Jaji  Mkuu  (Mst.  Zanzibar)  Hamid  Mahmoud  Hamid  amesema  kuwa,  Tume  inaendesha uchaguzi huo baada ya kupokea  barua  kutoka  kwa  Spika  wa  Bunge  la  Jamhuri  ya  Muungano  Mh.  Job  Ndugai kuhusu  uwepo  wazi  wa  jimbo  la  Kinondoni  jijini  Dar  es  Salaam  na  Jimbo  la  Siha  mkoani  Kilimanjaro.

Jaji  Mahmoud amesema  kuwa,  barua  hiyo  ilieleza  kuwa  majimbo  hayo  yapo  wazi  baada   Maulid  Mtulia   aliyekuwa  Mbunge  wa Jimbo  la  Kinondoni  kujivua  uanachama  wa  CUF  na  Dr.  Godwin  Mollel  wa  jimbo  la  Siha  kujiuzulu  uanachama  wa  CHADEMA  na  hivyo  wote  kukosa  sifa  za  kuwa  Wabunge.

Pia,  ameeleza kuwa Tume  ilipokea  taarifa  kutoka  kwa  Waziri  mwenye  dhamana  ya  Serikali  za  Mitaa  ikiitaarifu  Tume   uwepo  wa  nafasi  wazi  za  Udiwani katika  kata  nne  za  Tanzania  Bara

“Baada  ya  kupokea  barua  hizo  Tume  kwa  kuzingatia  vifungu  vya  37(1)  na  46(2)  vya  Sheria  ya  Taifa  ya  Uchaguzi  sura  ya  343  pamoja  na  kifungu  cha  13(3)  cha  Sheria  ya  Uchaguzi  wa  Serikali  za  Mitaa  sura  ya  292  inatangaza  kuwa  majimbo  mawili  na  kata  nne  zipo  wazi”  alisema  Jaji  Mahmoud.

Ameeleza  kuwa, fomu  za  uteuzi  kwa  majimbo  hayo  mawili  na  kata  nne  itakuwa  kati  ya  tarehe  14  - 20  Januari,  2018,  uteuzi  wa  wagombea  utafanyika  tarehe  20/01/2018, na Kampeni  za  uchaguzi  mdogo  zitafanyika  kuanzia  tarehe  21/01 – 16/02/2018  na  siku  ya  uchaguzi  itakuwa  tarehe  17/02/2017.

Vilevile,  Jaji  Mahmoud  amevikumbusha  Vyama  vya  Siasa  na  wadau  wote  wa  uchaguzi  kuzingatia  sheria,  kanuni,  taratibu,  miongozo  na  maelekezo  yote  wakati  wa  uchaguzi  huo  mdogo.

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi