Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Naibu Waziri Khamis Awafariji Waathirika Katesh
Dec 11, 2023
Naibu Waziri Khamis Awafariji Waathirika Katesh
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Khamis Hamza Khamis akiwa kwenye ziara ya kukagua athari za maafa ya mafuriko na maporomoko ya tope Katesh Wilaya ya Hanang mkoani Manyara.
Na Mwandishi Wetu

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Khamis Hamza Khamis amewatembelea na kuwapa pole waathirika wa mafuriko na maporomoko ya tope eneo la Katesh Wilaya ya Hanang mkoani Manyara.

Pia, amefanya ziara ya kukagua na kujionea athari zilizotokea ambapo ameipongeza Serikali kwa hatua na jitihada ilizochukua tangu kutokea kwa maafa hayo Desemba 03, 2023 ikiwemo kuwasaidia.

Mhe. Khamis amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye aliamua kuahirisha safari yake Dubai alipokuwa akishiriki Mkutano wa Mabadiliko ya Tabianchi na kurejea nchini kuwatembelea na kuwafariji waathirika kwa maafa hayo.

 

Naibu Waziri amewapa pole waathirika hao wakiwemo waliopoteza ndugu na mali zao na kuwaomba wawe na moyo wa subira na kumshukuru Mungu katika kipindi hiki kigumu wanachopitia.

“Nimekuja kuwapa pole kwa maafa haya yaliyotokea, Serikali ipo nanyi na inaendelea kuwapatia huduma zikiwemo makazi ili mrejee katika hali mliyokuwa nayo mwanzoni,“ amesema.

 

Aidha, Naibu Waziri amewaomba wananchi kumshukuru na kuendelea kumuomba Mungu na kuwa na moyo wa subira ambapo amewatia moyo kwa yote yaliyotokea.

 

Ametoa wito kwa uongozi wa wilaya kuendelea kuwapa ushirikiano waathirika ambao idadi kubwa ni wanawake, wazee na watoto ikiwemo kufuatila familia zilizoathirika popote zinapokuwa ili ziendelee kupatiwa misaada.

 

Katika ziara hiyo Naibu Waziri ameambatana na Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Sendiga, Mkuu wa Wilaya ya Hanang, Mhe. Janeth Mayanja na viongozi mbalimbali wa Mkoa na Wilaya.

 

Mara baada ya kutokea kwa maafa hayo Serikali ilichukua hatua za haraka zikiwemo kuwapa hifadhi waathirika katika Shule ya Sekondari Katesh na kuendelea kuwapatia huduma. 

.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi