Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Wizara ya Maliasili na Utalii Yaagizwa Kutoa Kitalu cha Uwindaji wa Kitalii kwa Chuo
Aug 18, 2020
Na Msemaji Mkuu

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Constantine Kanyasu akimkabidhi  begi lenye vitendea kazi Mwenyekiti wa Bodi ya Magavana wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka, Prof. Faustine  Bee wakati wa hafla ya uzinduzi wa Bodi hiyo iliyofanyika jana katika chuo hicho kilichopo mkoani Kilimanjaro

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Constantine Kanyasu amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii kutoa kitalu cha Uwindaji wa Kitalii kwa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori Mweka  ili kitumike kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi wanaosomea masomo ya Uwindaji Bingwa (Professional Hunters)

Ametoa agizo hilo leo wakati akizindua Bodi ya Magavana ya Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka kilichopo katika wilaya ya Moshi, mkoani Kilimanjaro.

Mhe. Kanyasu amesema kitalu hicho cha uwindaji wa kitalii kitakisaidia chuo hicho kuzalisha wataalamu wenye sifa.

Naibu Waziri wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Mhe. Constantine Kanyasu akimkabidhi begi lenye vitendea kazi Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt.Aloyce  Nzuki  mara baada ya Uzinduzi wa Bodi ya Magavana ya Chuo Cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka  iliyofanyika  Mkoani Kilimanjaro.

Amesema kwa sasa Mabingwa wa Uwindaji wa Kitalii wanaofanya kazi hiyo hapa nchini  ni raia wa kigeni na baadhi ya  Wazawa waliopo  ni Wazee.

Amesema kitalu hicho kitachochea kupata Wataalamu wa kutosha ili kuweza kukabiliana na uhaba wa Wataalamu wa fani hiyo.

Naibu Waziri wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Mhe. Constantine Kanyasu akikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa Bodi ya Magavana wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka wakati wa uzinduzi wa hafla hiyo  iliyofanyika chuoni hapo mkoani Kilimanjaro.

Aidha, Mhe. Kanyasu amesema chuo hicho kitasaidia kukabiliana na Wafugaji wanaoingiza vitalu vya uwindaji wa kitalii  kwa vile vitalu vingi  bado vipo wazi hali inayopelekea Wafugaji wengi  kuingiza mifugo hivyo.

Pia, Amesema Kitalu hicho hakitasaidia Wahitimu pekee kufanya mafunzo kwa vitendo bali itasaidia Wanyamapori kuwa salama kwa sababu chuo hicho kitakuwa na jukumu la kupambana na tatizo la ujangili.

Aidha, Mhe. Kanyasu amempongeza Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Prof. Faustine Bee kwa kuchaguliwa kwa awamu ya pili kuwa Mwenyekiti wa Bodi hiyo pamoja na Magavana wa Bodi kwa asilimia kubwa kuteuliwa tena kuendelea kukitumia chuo hicho.

Naibu Waziri wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Mhe. Constantine Kanyasu akiwa katika picha ya pamoja na baadhi  ya Magavana wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka kilichopo mkoani Kilimanjaro  mara baada ya kuzindua Bodi ya Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka, Wengi ni Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii. 

Awali, Mkuu wa chuo hicho, Prof. Jaffari Kidegesho amesema kwa sasa wanafunzi wa chuo hicho wamekosa maeneo ya kufanyia mafunzo kwa vitendo kwa ajili ya uwindaji wa kitalii.

Amesema mwanzo chuo hicho kilikuwa kikiyatumia mapori ya Akiba kwa ajili ya mafunzo hayo ila kwa sasa mapori hayo yamepandishwa hadhi na kuwa Hifadhi za Taifa hivyo katika Hifadhi hizo hakuna shughuli za kibindamu zinazoruhusiwa kufanyika kwa mujibu wa sheria.

Naye, Mkuu wa Chuo cha Wanyamapori, Mweka, Prof. Jaffari Kidegesho amesema kitalu hicho kitasaidia kufanya mafunzo kwa vitendo na hivyo kutasaidia kuwaandaa wahitimu wenye sifa kulingana na mahitaji ya soko

Naye, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Aloyce Nzuki amekitaka Chuo hicho kuboresha mtaala wa mafunzo hayo ili kuzalisha Wataalamu wataoweza kujibu changamoto za soko.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kilimanjaro, Alhaji Rajabu Kundya  amesema suala la uhifadhi na utalii limekuwa na mchango mkubwa sana kwa uchumi wa Taifa hali iliyopelekea Tanzania kuwa na Uchumi.

Amesema shughuli hizo wanazichukulia kwa uzito mkubwa na wanakithamini sana chuo hicho kwa mchango mkubwa wa kuzalisha wasomi wenye weledi.

Itakumbukwa kuwa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori Mweka ndo chuo pekee nchini kinachotoa mafunzo ya Uwindaji Bingwa wa Kitalii (PH)

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi