Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano Waongeza Mapato ya Serikali
Oct 15, 2018
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_36830" align="aligncenter" width="750"] Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano (wa pili kushoto) Mhandisi Atashasta Nditiye akikagua tundu la Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano kituo cha Rusumo linalopeleka mawasiliano kutoka Tanzania kwenda Rwanda. Mwenye koti nyeusi ni Mkurugenzi wa TEHAMA, Wizarani, Mulembwa Munaku na wa nne kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Ngara, Luteni Kanali, Michael Mntenjele[/caption]

Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano umeongeza makusanyo ya mapato ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye maeneo ya mipakani mwa Tanzania na nchi jirani za Rwanda, Uganda, Burundi na DRC Congo

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye wakati wa ziara yake ya kukagua Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano kwenye kituo cha mpakani cha Mtukula ambacho kinawezesha usafirishaji wa taarifa na data za wateja na bidhaa kutoka Tanzania kwenda nchi jirani ya Uganda.

Nditiye amesema kuwa, “maeneo ya mipakani ndio lango la kuongeza mapato na kukuza uchumi wa nchi yetu, niwatake muendelee na kasi hii ya ukusanyaji wa mapato ya Serikali kwa kutumia Kituo cha Pamoja cha Huduma ambapo tayari kwa kipindi cha miezi mitatu ya mwanzo wa mwaka wa fedha wa 2018/2019, mwezi Julai hadi Septemba, 2018 mapato yameongezeka zaidi ya asilimia 100 kwa mwezi na kufikia asilimia 150”.

Naye Afisa Mfawidhi wa Forodha wa Kituo cha Huduma cha Pamoja cha Mtukula, Bwana Mohammed Shamte amesema kuwa katika mwaka wa fedha wa 2018/2019, malengo yao ni kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 15.9 kwa mwaka ambapo tayari imeonekana kiwango hicho kitafikiwa kwa kuwa tayari kwa mwezi wanakusanya shilingi bilioni 1.3 ambazo ni wastani wa asilimia 110 hadi 150 ya makusanyo kwa mwezi ambayo yanavuka malengo. “Baada ya Serikali kuweka Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano, umeongeza spidi na uhakika wa kusafirisha taarifa na data tofauti na hapo awali tulipokuwa tunatumia satelaiti, hivyo Mkongo umewezesha ongezeko la mapato”, amesema Shamte.

[caption id="attachment_36831" align="aligncenter" width="750"] Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (kulia) akipata maelezo kuhusu Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano kutoka kwa Mhandisi wa Usafirishaji Masafa wa TTCL, Marwa Chacha wakati wa ziara yake ya kukagua namna Mkongo huo unavyopeleka mawasiliano Burundi kwenye kituo cha Biharamulo, Kagera[/caption]

Nditiye ameongeza kuwa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano umebadilisha sekta ya mawasiliano nchini na kwenye nchi za jirani zilizounganishwa na Mkongo huo za Uganda, Rwanda, Burundi, Kenya na DRC Congo ambapo wanafurahia huduma za mawasiliano. “Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano lazima ulindwe, ni kama reli au barabara, na mawasiliano ni uchumi na maendeleo ambapo unaingiza mapato kwa Serikali yetu,” amesema Nditiye

Pia, amewataka wafanyakazi wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL Corporation) waendelee kuutunza na kuendesha Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano kwa kuwa ni watu sahihi, wana utaalamu na ujuzi wa kutosha kufanya kazi na Serikali imewaamini na kuwapa jukumu hilo kwa kuwa mawasiliano ni uchumi na ni usalama hivyo ukicheza na mawasiliano nchi inasambaratika.

Wakiwasilisha changamoto za mawasiliano kwa Nditiye, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Misenyi Bi. Thabitha Solomoni amesema kuwa wakati mwingine mtandao unakwenda taratibu au kukosekana hivyo kuathiri usafirishaji wa taarifa na data za watumishi kwa Serikali wa malipo na masuala ya watumishi

[caption id="attachment_36832" align="aligncenter" width="750"] Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (wa kwanza kulia) akioneshwa ramani ya Tanzania na Mkurugenzi wa TEHAMA, Wizarani Bwana Mulembwa Munaku (wa kwanza kushoto) ya namna Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano ulivyoenea na kupeleka mawasiliano nchi jirani za Rwanda, Burundi, Uganda na DRC Congo wakati wa ziara yake kwenye kituo cha Mkongo, Biharamulo, Kagera[/caption]

Naye Meneja wa TTCL Mkoa wa Kagera Bi. Irene Shayo amejibu changamoto hio kwa kusema kuwa inategemea aina ya kifurushi ambacho Halmashauri husika imenunua na wanachotumia. Ametoa rai kwa Halamshauri kutumia wataalamu wao kufahamu uwezo wa mtandao wa intaneti wanaotumia ili uweze kuendana na mahitaji na ukubwa wa taarifa au data wanazotuma au kupokea, hivyo Ofisi za Serikali zizingatie ubora wa huduma kuendana na mahitaji yao na TTCL ina ofisi zake nchi nzima, wako tayari kuwahudumia.

Nditiye amepokea changamoto hiyo kuhusu spidi ya intaneti kwenye ofisi zao na amewataka wataalamu wa TEHAMA  kupeleka mahitaji sahihi ya mtandao wa intaneti kwa Wakurugenzi wa Halmashauri zao na TTCL wako tayari kushauri ili mahitaji yanayotakiwa yaweze kutolewa na TTCL kuendana na mahitaji stahiki

Naye Mkurugenzi wa TEHAMA, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Bwana Mulembwa Munaku amewataka maafisa TEHAMA wote kufungia mitandao ya kijamii muda wa saa za kazi ili mtandao wa intaneti uweze kutumika vizuri kwa matumiz ya Serikali

[caption id="attachment_36833" align="aligncenter" width="750"] Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (wa kwanza kulia) akipata maelezo kutoka kwa Afisa Mfawidhi wa Forodha wa Kituo cha Huduma cha Pamoja, Mtukula Bwana Mohammed Shamte (wa pili kulia) kuhusu namna Mkongo wa taifa wa Mawasiliano unavyowawezesha kusafirisha taarifa na data za wateja na bidhaa baina ya Tanzania na Uganda wakati wa ziara yake Mtukula, Kagera[/caption]

Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Brigedia Jenerali Marco Gaguti amemweleza Nditiye kuwa bado hakuna mawasiliano ya kuridhisha kwenye maeneo mbali mbali ya mkoa huo licha ya kwamba makampuni yote ya mawasiliano yapo ila bado kuna changamoto ya upatikanaji wa mawasiliano ya uhakika kwenye mkoa huo

Akitoa ufafanuzi kuhusu changamoto hiyo, Nditiye amesema kuwa tayari Serikali imechukua hatua kuhusu jambo hilo kwa kuongeza minara ya mawasiliano kwenye maeneo ya mipakani ambapo mawasiliano ni hafifu kwa kuwaelekeza wataalamu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote kufika kwenye maeneo hayo, kufanya tathmini na kupeleka mawasiliano kwa kuwa hadi sasa watanzania wanapata mawasiliano kwa kiwango cha asilimia 94 isipokuwa maeneo machache. Pia ameipa TTCL mwezi mmoja kuhakikisha vocha na laini za TTCL zinapatikana nchi nzima ili kuwawezesha watanzania kuwasiliana kwa kuwa mawasiliano ni uchumi na ni usalama

Nditiye amefanya ziara hiyo ya kukagua miundombinu ya Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano kwenye vituo vya mpakani vya Kabanga, Rusumo Mtukula na Biharamulo

Imetolewa na kitengo cha Mawasiliano Serikalini,

Wizara ya Ujenzi, uchukuzi na Mawasiliano

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi