Na Shamimu Nyaki
Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Pauline Gekul amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuibua na kukuza vipaji kupitia sekta zake.
Mhe. Gekul amesema hayo katika Mkutano wa Hadhara wa Rais Mhe. Samia uliofanyika leo Novemba 23, 2022 katika Uwanja wa Kwaraa mjini Babati ambapo amesema Takriban Shilingi bilioni 2 zimetengwa kwa mwaka huu wa fedha kwa ajili ya Mfuko wa Utamaduni na Sanaa.
"Halmashauri ya Mji wa Babati imetumia takriban Shilingi milioni 95 kujenga uzio katika Uwanja huu wa Kwaraa mjini hapa, naomba nitumie nafasi hii kutoa wito kwa Halmashauri zote nchini kutenga fedha za mapato ya ndani kwa ajili ya kukarabati na kujenga miundombinu ya michezo", amesema Mhe. Gekul.
Ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita, kwa kutenga fedha takriban Shilingi bilioni 300 kwa ajili ya kusaidia timu za Taifa ambazo zimesaidia timu ya Taifa ya Walemavu ya Tembo Worrios na Timu ya Taifa ya Wanawake chini ya Miaka 17 (Serengeti Girls) ambazo zote zimefuzu Kombe la Dunia na kufika hatua ya Robo Fainali.