Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Mfumuko wa Bei Mwezi Juni Waendelea kuwa Asilimia 3.2
Jul 08, 2020
Na Msemaji Mkuu

Na   Mwandishi Wetu- MAELEZO

Mfumuko wa bei wa Taifa kwa  mwezi Juni 2020 umeendelea kuwa asilimia 3.2 kama ilivyokuwa mwezi  Mei, 2020.

Akizungumza leo Julai 8, 2020 Jijini Dodoma,  Kaimu Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Takwimu za Jamii kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Bi. Ruth Minja amesema kuwa hali hiyo inamaanisha kuwa kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma kwa mwaka unaoishia mwezi Juni umebaki kuwa sawa na iliyokuwepo kwa mwezi Mei.

Akifafanua, Bi Minja amesema kuwa baadhi ya bidhaa za vyakula zilipungua bei kwa mwezi Juni 2020 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka 2019, baadhi ya bidhaa hizo ni pamoja unga wa mahindi kwa asilimia 1.6, matunda kwa asilimia 2.1, viazi mviringo asilimia 0.5 na mihogo asilimia 13.3.

Kwa upande wa bidhaa zisizo za vyakula amesema kuwa ziliongezeka bei kwa mwezi Juni, 2020 ikilinganishwa na bei za mwezi Juni 2019, bidhaa hizo ni pamoja na mavazi kwa asilimia 2.7, gesi ya kupikia kwa asilimia 7.8 , mkaa asilimia 11.2, samani asilimia 2.7 na vitabu vya shule kwa asilimia 1.5.

Mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa mwaka ulioishia mwezi Juni, 2020 umepungua hadi asilimia 3.8 kutoka asilimia 4.4 kwa mwaka unaoishia mwezi Mei, 2020.

Kwa upande wa nchi ya Kenya Bi Minja amesema kuwa Mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia mwezi Juni, 2020 umepungua hadi kufikia asilimia 4.59 kwa mwaka ulioishia mwezi Mei, 2020. Kwa upande wa Uganda, Mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia mwezi Juni, 2020 umeongezeka hadi asilimia 4.1 kutoka asilimia 2.8 kwa mwaka ulioishia mwezi Mei, 2020.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi