Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Mfumo wa PlanRep Kuanza Kutumika Bajeti ya 2018/2019.
Aug 09, 2017
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_8742" align="aligncenter" width="750"] Muwezeshaji kutoka Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Archibold Kundasai (aliyesimama) akimuelekeza mmoja wa washiriki wa mafunzo ya Mfumo ulioboreshwa wa kuandaa Mpango wa Bajeti za Mamlaka ya Serikali za Mitaa (PlanRep) namna ya kujiunga na mfumo huo kwenye mtandao. Mafunzo hayo ya siku 8 yaliyofadhiliwa na USAID yanaendelea mjini Morogoro.[/caption]

Na Jacquiline Mrisho, Morogoro.

Mfumo ulioboreshwa wa kuandaa Mpango wa Bajeti za Mamlaka ya Serikali za Mitaa (PlanRep) unatarajiwa kuanza kutumika rasmi kwenye maandalizi na utekelezaji wa Bajeti ya mwaka 2018/2019.

Hayo yamebainishwa leo mjini Morogoro na Mkurugenzi Msaidizi wa Miundombinu ya TEHAMA – TAMISEMI, Baltazar Kibola wakati mafunzo ya mfumo huo yakiendelea mjini humo.

Kibola amesema kuwa bado watumiaji wa mfumo huo wanaendelea na mafunzo katika baadhi ya Kanda hivyo hadi kufikia kwenye maandalizi ya Bajeti ya mwaka 2018/2019 maafisa wanaohusika na upangaji wa bajeti na mipango ya Serikali watakuwa wameshafahamu namna ya kutumia mfumo, pia Mikoa na Halmashauri zote zitakuwa zimeshaunganishwa na mfumo huo.

[caption id="attachment_8755" align="aligncenter" width="750"] Muwezeshaji kutoka Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Archibold Kundasai (aliyesimama kulia) akiangalia jinsi washiriki wa mafunzo ya Mfumo ulioboreshwa wa kuandaa Mpango wa Bajeti za Mamlaka ya Serikali za Mitaa (PlanRep) wanavyofanya mazoezi ya matumizi ya mfumo huo. Mafunzo hayo ya siku 8 yaliyofadhiliwa na USAID yanaendelea mjini Morogoro.[/caption]

“Hadi kufikia Oktoba mwaka huu wakati tunaanza maandalizi ya Bajeti za 2018/2019, mfumo huu utakuwa tayari kwa ajili ya matumizi pia wakati wa utekelezaji wa bajeti hiyo tutakuwa tumeshauwezesha mfumo huo kupatikana hata sehemu zenye changamoto ya mtandao”, alisema Kibola.

Amefafanua kuwa ili kuweza kutumia mfumo huo ni lazima kifaa cha mtumiaji kiwe kimeunganishwa katika mtandao lakini kwa kuwa sehemu nyingi zina changamoto hiyo, mfumo huo utaboreshwa ili kumuwezesha mtumiaji kujaza taarifa katika mfumo hata kama hajaunganishwa na mtandao lakini wakati wa kutuma taarifa hizo lazima atahitaji kuwa na mtandao.

Kwa upande wake mmoja wa waliohudhuria mafunzo, Mchumi wa Manispaa ya Moshi, Anganile Mwasongwe amesema kuwa mfumo huo umerahisisha kazi ya upangaji wa Bajeti kwa sababu unamruhusu muhusika kuripoti kila kitu anachokifanya kwa muda mfupi hali itakayopelekea urahisi wa kufahamu upangaji wa Bajeti na mipango mingine ya Serikali pamoja na uwajibikaji wa afisa husika.

[caption id="attachment_8756" align="aligncenter" width="750"] Muwezeshaji ambaye pia ni Mchumi wa Mkoa wa Kilimanjaro, Apolinary Seiya (aliyesimama) akiendelea na mafunzo ya Mfumo ulioboreshwa wa kuandaa Mpango wa Bajeti za Mamlaka ya Serikali za Mitaa (PlanRep) kwa watumiaji wa mfumo huo leo mkoani Morogoro.[/caption]

“Katika kipindi hiki cha kuipeleka Serikali kutumia mifumo ya kielektroniki tunawaomba wawezeshaji wa mafunzo wawe wanachukua maoni yetu na kuyafanyia kazi ili waweze kuboresha zaidi mifumo hiyo kwa sababu sisi ndio tutakaoenda kuitumia hivyo ikiwa haiko sawa kazi hazitofanyika kwa urahisi”, alisema Mwasongwe.

Mafunzo haya ya siku 8 yamefadhiliwa na Shirika la Msaada la Marekani (USAID) chini ya mradi wa miaka mitano ulioanza mwaka 2015 hadi 2020 unaohusisha maafisa wa Serikali wanaotumia mfumo wa PlanRep wakiwemo; Waganga Wakuu, Makatibu wa Afya, Maafisa TEHAMA, Wachumi, Wahasibu na Maafisa Mipango.

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi