[caption id="attachment_4606" align="aligncenter" width="750"] Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akihutubia wakati wa Uzinduzi wa Mwongozo kwa Wapelelezi na Waendesha Mashitaka wa Kesi za Wanyamapori na Misitu kwenye ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam. (Picha na: OMR)[/caption]
Na: Mwandishi Wetu
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amewaagiza wapelelezi na waendesha mashtaka nchini kuepuka vitendo vya rushwa na badala yake wafanye kazi kwa bidii kwa kuweka mbele maslahi ya taifa.
Makamu wa Rais ametoa agizo hilo wakati akizindua mwongozo kwa wapelelezi na waendesha mashtaka wa kesi za wanyamapori na misitu. Uzinduzi huo umefanyika leo katika Lituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius kilichopo Jijini Dar es Salaam amabpo amewataka wapelelezi na waendesha mashtaka kuchukua hatua stahiki dhidi ya watu wanaoiba rasilimali za taifa.
Amesema mwongozo aliouzindua utasaidia kwa kiwango kikubwa Kuboresha shughuli za upelelezi na uendeshaji wa kesi zinazohusu wanyapori na misitu nchini.
[caption id="attachment_4609" align="aligncenter" width="750"]“Uwepo wa mwongozo huu ni dhahiri unategemewa kutoa matokeo chanya katika mapambano dhidi ya ujangili na uhalifu misitu yetu”, alisisitiza Makamu wa Rais.
Mhe. Samia Suluhu Hassan ameeleza imani yake kuwa mwongozo huo aliouzindua utasaidia kukomesha vitendo uhalifu ambavyo vimekuwa vikiisababishia Serikali hasara kubwa, ikiwemo uharibifu wa rasilimali za taifa na kupoteza mapato ambayo yangesaidia kuimarisha huduma za jamii nchini.
Kuhusu sekta ya utalii nchini, Makamu wa Rais amesema pamoja na sekta hiyo kuliingizia taifa mapato mengi lakini inasikitisha kuona kuwa wanyamapori ambao ndio nguzo kuu ya sekta ya utalii wanazidi kupungua kila kukicha hivyo kutishia uchumi na nchi.
“Wazee wetu walizilinda na kuzitunza rasilimali zetu kwa faida yetu, nasi tuzitunze kwa ajili ya vizazi vijavyo”, alieeleza Makamu wa Rais
Kwa upande wake, Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe amemhakikishia Makamu wa Rais kuwa kazi ya kupambana na ujangili na utoroshaji holela wa wanyama na viumbe wengine itakuwa endelevu na wale wote watakaokamatwa watachukuliwa hatua kali za kisheria ili kukomesha vitendo hivyo.
[caption id="attachment_4609" align="aligncenter" width="750"]Profesa Maghembe amemuomba Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini kuendesha oparesheni ya maalum ya kukusanya silaha zote ambazo zimekuwa zikitumika kwenye ujangili ili kuhakikisha wanyama hasa tembo wanakuwa salama kwenye maeneo ya hifadhi za Taifa nchini.
Naye, Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali, Biswalo Mganga amefafanua kuwa katika kipindi cha mwaka 2014/2017 ofisi yake imewafikisha mahakamani washtakiwa wakubwa wa ujangili ambao walikuhumiwa vifungo virefu na faini, ambapo washtakiwa 100 kati yao walihukumiwa kulipa faini ya zaidi ya shilingi bilioni 1.1 kwa kukutwa na nyara za Serikali kinyume na sheria na kwamba faini hizo zimehalipwa Serikalini.
Ameeleza kuwa kati ya idadi hiyo watuhumiwa zaidi ya 80 walihukumiwa kifungo cha miaka 20 hadi 30 gerezani na faini ya zaidi ya shilingi milioni 164 ambazo bado hazijalipwa Serikalini.
[caption id="attachment_4610" align="aligncenter" width="750"]Bw. Biswalo alisema mafanikio hayo yote yamechangiwa na usimamizi madhubuti wa kesi hizo kupitia dawati la wanyamapori katika Divisheni ya Mashtaka pamoja na Mawakili wa Serikali katika Ofisi zote za mikoani nchini.
Aidha, alieleza kuwa changamoto kubwa wanayokutana nayo kwenye kazi kwa sasa ni dhamana kwa watuhumiwa wakubwa wa vitendo vya ujangili ambapo utafiti uliofanywa Mahakama za mkoa wa Dar es salaam tu katika kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015 unaonyesha kuwapo kwa jumla ya mashauri 13 yanayohusishwa na nyara za Serikali zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 800 zilizokamatwa ndani na nje ya nchi ambapo watuhumiwa wake walipewa dhamana na kutoweka.
Biswalo Mganga amesema katika mashauri hayo asilimia 69 walikuwa ni raia wa kigeni na asilimia 31 ni raia wa Tanzania.