Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Kiwanda cha Kagera Sugar Chatoa Kodi ya bilioni 44 kwa Miaka mitatu
Sep 07, 2018
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_34956" align="aligncenter" width="900"] Waziri wa Viwanda Biashara na Uwekezaji Mhe. Charles Mwijage akisisitiza kuhusu hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kuondoa changamoto zilizopo katika sekta ya sukari hapa nchini ili kuwalinda wananchi na kuhakikisha kuwa biashara ya sukari inafanyika kwa kuzingatia sheria na kanuni.[/caption]

Na Jacquiline Mrisho.

Kiwanda cha Sukari cha Kagera kimeilipa Serikali kodi ya jumla ya shilingi 44,461,815,798 katika kipindi cha miaka mitatu tangu 2015 hadi 2018.

Takwimu hizo zimetolewa leo na Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Nkenge, Balozi Dkt. Diodorus Kamala lililohoji manufaa ya kiwanda cha Sukari cha Kagera kwa wananchi wa Wilaya ya Misenyi, Mkoa wa Kagera na Taifa kwa ujumla.

Waziri Mwijage amesema kuwa tangu kiwanda hicho kibinafsishwe,faida na michango mbalimbali imepatikana ikiwemo ya kuongezeka kwa uzalishaji wa sukari kutoka tani 15, 362 zilizozalishwa mwaka 2004/05 hadi kufikia tani 75, 568 mwaka 2017/18 ambapo uzalishaji huo umesaidia kuokoa fedha za kigeni ambazo zingetumika kuagiza bidhaa hiyo toka nje ya nchi.

"Mpaka sasa kuna wakulima 500 wanaolima eneo la hekari 5, 019 za miwa ambapo kwa Mwaka wa Fedha 2017/18 wakulima hao waliweza kuzalisha tani 60,000 za miwa zilizowapatia kipato cha shilingi bilioni kuwepo kwa kiwanda hiki ni faida kwetu hivyo natoa rai kwa wafanyabiashara wa sukari kuendelea kuzingatia sheria za kuendesha biashara hiyo,"alisema Mwijage.

Waziri Mwijage ameongeza kuwa hadi kufikia mwaka 2018, kiwanda kimetoa jumla ya ajira 6,000, kimejenga hospitali yenye vitanda 78, kimechangia vifaa vya ujenzi wa madarasa, kimechimba visima vya maji, kujenga vyoo, nyumba za walimu pamoja na madawati.

Vile vile kiwanda hicho kimechangia ujenzi wa maabara na kutoa vifaa vya kufundishia kwa shule 23 katika Wilaya ya Misenyi, kimepanda jumla ya miti 20,000 katika eneo la kiwanda hicho pia kimejenga mtandao wa barabara zenye urefu wa Kilomita 1,250.

Aidha, Waziri Mwijage amefafanua kuwa kiwanda hicho kina utaratibu wa kuwatumia wakulima wa nje katika kulima miwa inayotumia hivyo inawaletea manufaa wakulima nchini kwa kulima mazao bora yenye tija.

Kiwanda cha Sukari cha Kagera ni kati ya Viwanda vilivyobinafsishwa katika miaka 90 kikiwemo cha  Kilombero kilichopo mkoani Morogoro. Hivi karibuni Mhe. Rais John Pombe amekuwa akisisitiza kuwa viwanda vilivyobinafsishwa na  hadi sasa havifanyi kazi virudishwe Serikalini.

   

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi