Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Kitabu cha ‘SOTE TUNAWEZA’ Kusaidia kukuza Kiswahili
Dec 22, 2017
Na Msemaji Mkuu

[caption id="attachment_25468" align="aligncenter" width="750"] Mkurugenzi Mtendaji na Mwanzilishi wa VIVA lEGACY lTD (t) Bi. Fortunata Meela Temu akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu uzinduzi wa kitabu chaake cha "SOTE TUNAWEZA" leo Jijini Dar es Salaam. Kutoka kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Habari (MAELEZO) Rodney Thadeus, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Avemaria Semakafu na Mwajiri Msaidizi wa Viva Legacy (T) Ltd Bi. Neema Seleman.[/caption]

Na Jacquiline Mrisho.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu amesema kitabu cha ‘SOTE TUNAWEZA’ kitakuza na kuenzi lugha ya Kiswahili kwa sababu kimeandikwa kwa lugha ya Kiswahili fasaha na rahisi kueleweka kwa wasomaji.

Ameyasema hayo leo Jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu maudhui na lengo la kitabu hicho kilichoandikwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Viva Legacy Limited, Bi. Fortunata Temu.

Dkt. Ave Maria amesema kitabu hicho kimekuja katika wakati muafaka kwa sababu nchi inapita katika kipindi cha mabadiliko ya kuelekea katika uchumi wa viwanda hivyo katika harakati hizo lazima wananchi wabadili fikra na mitazamo kuhusu viwezesho vya mafanikio.

[caption id="attachment_25469" align="aligncenter" width="750"] Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Avemaria Semakafu (katikati) akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu uzinduzi wa kitabu chaake cha "SOTE TUNAWEZA" leo Jijini Dar es Salaam. Kutoka kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Habari (MAELEZO) Rodney Thadeus, na Mkurugenzi Mtendaji na Mwanzilishi wa VIVA lEGACY lTD (t) Bi. Fortunata Meela Temu.[/caption]

“Katika nchi yetu suala la uandishi wa vitabu kwa kiasi fulani umerudi nyuma, tumekuwa tukitegemea kusoma vitabu kutoka nje ya nchi hivyo tuitumie hii kama fursa ya sisi kuandika vitabu vyenye maudhui na vyenye kutumia lugha ya Kiswahili ili kuikuza lugha yetu,” alisema Dkt. Ave Maria.

Dkt. Ave Maria ameongeza kuwa kitabu hicho kimetumia lugha ya Kiswahili hivyo faida nyingine inayopatikana katika kitabu hicho ni kulisaidia Taifa katika kukuza utamaduni wa kitanzania kupitia kukienzi Kiswahili kwa maandishi.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Viva Legacy Limited na Mwandishi wa kitabu hicho, Bi. Fortunata Temu amesema lengo la kitabu hicho ni kuchangia uimarishaji wa mifumo ya kiutendaji na hasa kuboresha rasilimali watu.

“Kitabu hiki kinampa msomaji hamasa ya kubadili fikra na mitizamo kuhusu viwezesho vya mafanikio kwa kumjengea uwezo wa uelewa wenye kumsukuma Mtanzania kuelekea kwenye safari ya mafanikio iliyostawi ndani ya utajiri wa akili na mali,” alisema Bi. Fortunata.

[caption id="attachment_25470" align="aligncenter" width="750"] Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia  Dkt. Avemaria Semakafu (kulia) pamoja na Mkurugenzi Mtendaji na Mwanzilishi wa VIVA Legacy Ltd (T) Bi. Fortunata Meela Temu wakiwaonyesha Waandishi wa Habari kitabu cha "SOTE TUNAWEZA" leo Jijini Dar es Salaam. Kitabu hicho kimetungwa kwa lengo la kuimarisha mfumo wa utendaji na hasa kuboresha rasilimali watu.[/caption][caption id="attachment_25471" align="aligncenter" width="750"] Baadhi ya Waandishi wa Habari wakifuatilia mkutano baina yao na na Mkurugenzi wa Viva Legacy (T) Ltd alipokuwa akizungumzia kuhusu uzinduzi wa kitabu cha SOTE TUNAWEZA leo jijini Dar es Salaam. (Picha zote na: Frank Shija)  [/caption]

Aidha, Bi. Fortunata amesema kuwa matumizi ya lugha ya Kiswahili katika kitabu hicho ni mkakati mahususi wa kuchangia kueneza matumizi ya lugha hiyo adhimu ndani na nje ya nchi kwani soko la Kiswahili linakua kwa kasi.

Katika kukienzi na kukithamini Kiswahili, hivi karibuni ilizinduliwa Kamusi mpya ya lugha hiyo ambayo imejumuisha maneno mapya na yaliyotoholewa pamoja na misamiati mipya ambayo haikuwemo katika Kamusi zilizopita.

Lugha ya Kiswahili pia imeendelea kutumika kwenye shughuli mbalimbali za Kitaifa na Kimataifa na kwa mujibu wa tafiti ni miongoni mwa lugha kuu tatu kwa kuwa na watumiaji wengi katika Bara la Afrika.

 

 

 

 

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi