Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Dkt. Mwigulu Aitaka TRA Kusaidia Kukuza Sekta Binafsi Nchini
Oct 03, 2023
Dkt. Mwigulu Aitaka TRA Kusaidia Kukuza Sekta Binafsi Nchini
Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu, akizugumza na wananchi wa Kitongoji cha Kilambo, Kata ya Njisi, Wilani Kyela (Hawapo pichani) mara baada ya kutembelea na kukagua shughuli za kiuchumi na maendeleo katika mpaka wa Tanzania na Malawi wa Kasumulu, mkoani Mbeya. Kulia kwake ni Waziri wa Ujenzi, Mhe. Innocent Bashungwa na kushoto ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Wilaya ya Kyela,Bw. Elias Mwanjala.
Na Ramadhani Kissimba, WF, Kyela

Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, ameiagiza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kusaidia kukuza Sekta Binafsi nchini ambayo itasaidia kuongeza kipato, kukuza uchumi wa nchi na itatoa fursa kwa vijana wengi kujiajiri.

Mhe. Dkt. Nchemba alitoa maagizo hayo leo Oktoba 03, 2023 wakati akiongea na wananchi wa Kilambo, Kata ya Njisi, wilayani Kyela, Mkoani Mbeya, mara baada ya kufanya ziara yake ya kukagua shughuli za kiuchumi na maendeleo katika Kituo cha Forodha cha Pamoja-Kasumulu kilichopo mpakani mwa Tanzania na Malawi.

"Ni lazima tuwe na nidhamu katika kuisaidia sekta binafsi na tuache ubosi katika mitaji ya watu na kama kijana ameamua kuanzisha shughuli yake na hajaisajili msimfungie biashara badala yake mleteeni hiyo leseni ambayo hana, msiharibu mtaji wake ili vijana wengi wajiajiri," alisema Mhe. Dkt. Nchemba

Aidha, Mhe. Dkt. Nchemba aliwataka wananchi kujenga tabia ya kulipa kodi na kuheshimu sheria za nchi ili kuongeza idadi ya walipa kodi, jambo ambalo litasaidia kushusha viwango vya ulipaji kodi na kuwapunguzia mzigo mkubwa wale wanaolipa kodi na kwamba matamanio ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa  Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ni kuona viwango vya kodi vinashuka ili kuchochea maendeleo ya kila Mtanzania.

"Natoa rai hapa wakati tunawasisitizia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kutekeleza maelekezo ya Mhe.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kukusanya mapato kwa weledi na kufuata kanuni, tunawasisitiza pia wananchi mjenge utaratibu wa kulipa kodi, kuheshimu sheria ili tunapokwenda tukilipa wengi, tuweze kushusha viwango vya kodi’’ Aliongeza Mhe. Dkt. Nchemba.

Awali akizungumza na Uongozi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Uongozi wa Jeshi la Polisi Mkoani Mbeya, Mhe. Dkt. Nchemba aliwataka kuhakikisha wanadhibiti na kuwachukulia hatua kali za kisheria wale wote wanaofanya biashara za magendo katika mpaka wa Kasumulu, vitendo vinavyoikosesha Serikali mapato.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi