Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Blogu ya Idara ya Habari - MAELEZO

Dkt. Chaula Ataka Uwajibikaji Vyuo vya Maendeleo ya Jamii
Mar 18, 2022
Na Jacquiline Mrisho

Na WMJJWM Iringa

Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Zainab Chaula amewataka watumishi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii Ruaha kuwa wabunifu na kufanya shughuli za kuwaletea maendeleo.

Dkt. Chaula ameyasema hayo leo alipotembelea chuoni hapo kukagua shughuli na miradi ya Maendeleo. 

Dkt. Chaula amesema Vyuo vya Maendeleo ya Jamii ni chachu ya maendeleo ya nchi hivyo, vitumike kuibua vipaji vya watumishi na wahitimu ili waweze kuzalisha kwa tija na hatimaye kujiletea maendeleo kiuchumi.

Akiwa chuoni hapo, Katibu Mkuu amezindua mradi wa ufugaji wa Samaki unaolenga kutumika kwa mafunzo kwa wanachuo na wakazi wa maeneo jirani.

Akizungumza kuhusu mradi huo, Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii Ruaha, Godfrey Mafungo amesema mradi unalenga kutoa elimu ya ufugaji wa Samaki kwa jamii na wanafunzi na kuwa moja ya chanzo cha mapato pale wanafunzi wanapohitimu wanapata fursa za kujiajiri na kuajiri.

Akitoa maelezo mbele ya mgeni rasmi, Mtaalam wa viumbe vya majini, Chande Mazola amesema mradi huo utaweza kuwakwamua wanajamii dhidi ya umasikini kwani wengi wao wameanzisha mabwawa ya ufugaji wa Samaki na kuweza kuuza kwenye maeneo yao na nje ya vijiji vyao ili kuongezea kipato cha mtu mmoja mmoja.

Awali akiuzungumzia uanzishwaji wa miradi, Katibu Mkuu Dkt. Chaula amesema, miradi ya aina hiyo ni mbinu mojawapo ya kumhudumia mwananchi hasa makundi maalum ambayo yanahudumiwa na Wizara kujikwamua kiuchumi.

Baadhi ya watumishi Ruaha CDTI, wamepongeza Katibu Mkuu Chaula kwa kuwapa motisha ya kazi na kuwashirikisha maono ya kupata mafanikio na kuahidi kuyafanyia kazi maelekezo na ushauri waliopewa ili kukifanya Chuo hicho kuwa Cha manufaa na cha kuleta tija kwa wanafunzi na jamii inayoizunguka.

Mipangilio
Marekebisho ya Mandhari
Marekebisho ya Maandishi