Na WMJJWM, Dodoma
Katibu wa Wabunge vinara wa Ustawi wa Jamii Mhe. Justine Nyamoga amesema wapo tayari kushirikiana na Serikali kukemea vitendo vya ukatili kwenye jamii.
Mhe. Nyamoga ameyasema hayo Jijini Dodoma Juni 21, 2022 katika kikao kazi cha kuwajengea uwezo wabunge vinara wa Ustawi wa Jamii kuhusu utekelezaji, uendeshaji na usimamizi wa Afya mbalimbali za Ustawi wa Jamii katika ngazi ya Halmashauri.
“Sisi wabunge vinara tunawajibu wa kuwa mfano kwa jinsi ambavyo tunaenenda kwa kukataa vitendo vya ukatili na kupaza sauti kuhusu vitendo hivyo popote tutakapokuwa iwe ndani au nje ya Bunge katika kuiunga mkono Serikali yetu” amesema Nyamoga.
Nyamoga amepongeza pia hatua ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kuunda Wizara inayohusika na Masuala ya Ustawi wa Jamii pamoja na kuridhia katika ajira zinazotarajiwa kuwepo na Maafisa Ustawi wa Jamii ambapo amesema itasaidia kuondoa mkanganyiko uliokuwepo na kuimarisha utendaji.