NA OSCAR ASSENGA, TANGA.
Serikali ipo katika mazungumzo na Wawekezaji juu ya mpango wa ujenzi wa Bandari mpya ya Bagamoyo mkoani Pwani ili kusogeza huduma karibu na wananchi na hivyo kuchangia kukuza Pato la Taifa na wananchi kwa ujumla.
Hayo yalisemwa na Mkurugenzi wa Idara ya Habari – MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa wakati wa ziara ya Maafisa Habari wa Wizara na Taasisi za Umma nchini katika Bandari ya Tanga ambao wapo Jijini Tanga wakiendelea na kikao chao.
Alisema kwa sasa wamerejesha mazungumzo hayo baada ya Rais Samia Suluhu kupitia Serikali yake ya Awamu ya Sita kuona ni vyema wakarejesha mazungumzo hayo na kukubaliana maeneo serikali itayoona ina maslahi nayo pamoja na wawekezaji ili wautekeleze mradi huo.
Alisema mradi huo ni mkubwa na wakifanikiwa kuutekeleza utasaidia kuchochea kasi ya maendeleo na hivyo kuchangia pato la wananchi na Taifa kwa ujumla ikiwemo kufungua milango ya uwekezaji hapa nchini.
Alisema sio Bandari bali patajengwa Viwanda, kwa sababu eneo hilo wanakusudia kulifanya liwe kanda maalumu ya kiuchumi ya Bagamoyo ambapo patajengwa bandari, Viwanda, eneo la makazi, maduka makubwa na sehemu nyingi za kibiashara ikiwemo ujenzi wa viwanda takriban 1000 na hivyo itawezesha kuwa kanda maalumu ya viwanda.